LEMBELI kuihama CCM?, Mafuriko ya LOWASSA CHADEMA na Mwinyi avunja ukimya

MWANANCHI
Mbunge wa Kahama, James Lembeli ameiweka njiapanda CCM baada ya kutangaza kutogombea ubunge kwa tiketi ya chama hicho.
Uamuzi wa Lembeli umekuja wakati wanachama kutoka sehemu mbalimbali wakitangaza uamuzi wao wa kujiengua CCM na kujiunga na vyama vya upinzani, hasa Chadema ambayo imesomba asilimia kubwa ya wahamaji hao.
 Lembeli alisema taarifa hizo ni uvumi uliozagaa jimboni kwake, lakini hajajiunga na chama chochote.
“Ni uvumi tu na uvumi wenyewe umechangiwa na swali nililoulizwa leo na wananchi kwamba ‘mbona toka mchakato wa kuchukua fomu umeanza hatujakuona’ na mimi nikawajibu kuwa ‘sitachukua fomu’,” alisema.
Lembeli alisema amechukua uamuzi huo kutokana na rafu inayoendelea jimboni humo na maneno ya baadhi ya wanachama, wakiwemo viongozi kuwa hatakiwi na vigogo ndani ya CCM.
Lembeli, mmoja wa wabunge waliokuwa mstari wa mbele wakati wa kashfa ya uchotwaji fedha kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow, alisema sababu za kutotakiwa huko zinatokana na dhana potofu ya baadhi ya viongozi kwamba michango yake ndani na nje ya Bunge inaivua nguo Serikali.
“Tangu mchakato wa uchukuaji wa fomu umeanza baadhi ya wanachama wengi tu wameitwa kwenye vikao visivyo halali karibu kata zote wakiwa na kadi zao na kuorodheshwa na kupewa maagizo ya kunikataa kwenye kura ya maoni na wengine wanapewa Sh5,000,” alisema mwandishi huyo wa habari.
Lembeli alidai kuwa mbaya zaidi ni kwamba zipo kadi mpya za CCM zinazotolewa kiholela bila kufuata utaratibu na licha ya kulalamikia hali hiyo hakuna hatua zilizochukuliwa.
Alisema kutokana na yote hayo, aliwahi kusema kwenye mkutano wa hadhara kuwa kuna njama hizo, lakini badala ya CCM kufanyia kazi madai hayo, wakamuita mbele ya Kamati ya Maadili.
“Kwenye kamati ya maadili nilituhumiwa kuwa nakidhalilisha chama na kutakiwa niwataje nani walioniambia sitakiwi. Niliwajibu, tena kwa maandishi na kuwapa orodha, lakini mpaka leo kimya ina maana mimi bado ni mtuhumiwa,” alidai.
“Mimi siyo mtoto mdogo. Naelewa nini kinaendelea na ndiyo maana nimesema sitachukua fomu ya kugombea ubunge kwa mazingira haya. Bado sijatangaza kuhama CCM”.
Wakati Lembeli akisisitiza suala la kuhama kwake ni fununu tu, habari nyingine zilidai huenda akagombea ubunge kwa tiketi ya Chadema kutokana na kutokubaliana na mchakato huo anaodai ni batili.
MWANANCHI
Janeth Magufuli bado anasubiri miezi mitatu ya kampeni nzito za kumuwezesha mumewe kuingia kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano, lakini walimu na wanafunzi wa Shule ya Msingi Mbuyuni tayari wanasikitika kumpoteza mwalimu huyo wa jiografia, historia na Tehama.
Mumewe, Dk John Pombe Magufuli amepitishwa zaidi ya wiki moja iliyopita kuwa mgombea urais wa Tanzania kwa tiketi ya CCM, na hivyo atalazimika kupambana vikali na wagombea wa vyama vingine ili kujihakikishia anaingia Ikulu kuongoza Serikali ya Awamu ya Tano.
Lakini walimu na wanafunzi wa shule hiyo wanaona kuwa tayari Dk Magufuli ameshajihakikishia tiketi ya kuingia Ikulu na walichonacho sasa ni kusononeka kwa kuwa wanampoteza mmoja wa walimu bora shuleni hapo.
“Kama mumewe akichaguliwa, nitakosa utu na busara zake. Na unajua? Ni mwalimu wa mazingira na anajua majukumu yake. Darasa la tano watamkumbuka sana,”anasema mwalimu mkuu wa shule hiyo, Dorothy Malecela.
“Ni mwanamke mchapakazi sana na ni mwalimu mzuri, mtu mwenye upendo na mnyenyekevu. mtu pia mwenye moyo mzuri. Wakati fulani alitoa msaada wa baiskeli kwa mwanafunzi mlemavu shuleni hapa.”
Alikuwa akimzungumzia mwanafunzi mlemavu Elisha Lameck, ambaye alikuwa akipata shida kutoka sehemu moja kwenda nyingine wakati akiwa shuleni hapo.
Mwalimu Malecela anasema licha ya kuwa ni mke wa Waziri Magufuli, ilikuwa kazi kufahamu kama ni mke wa kigogo.
“Hakuwa na makuu hata kidogo, hata watoto wake walikuwa wakisoma hapa, na mwingine anasoma shule ya Kata ya Oysterbay,” anaeleza.
“Watoto wao wanasoma shule za kawaida sana. Shule ya kata tofauti na wengine ambao huwapeleka nje ya nchi.”
MWANANCHI
Rais mstaafu wa Awamu ya Pili, Alhaj Ali Hassan Mwinyi amesema kuwa shughuli ya kupata mgombea urais kwa tiketi ya CCM haikuwa rahisi na akashukuru kwamba imemalizika kwa amani.
Mchakato huo ulihitimishwa Julai 12 mjini Dodoma wakati Mkutano Mkuu wa CCM ulipopitisha jina la Dk John Magufuli kugombea nafasi ya kuongoza Serikali ya Awamu ya Tano baada ya Rais Jakaya Kikwete kumaliza muda wake mwishoni mwa mwaka.
Jumla ya makada 38 walijitokeza kuwania nafasi hiyo, na majina matano ndiyo yaliyopitishwa kwenda Halmashauri Kuu na baadaye matatu kwenda Mkutano Mkuu.
Mchakato wa urais ndani ya CCM ambao kwa kawaida hutawaliwa na msuguano kabla ya kumalizika kwa maridhiano, safari hii ulienda mbali zaidi baada ya wajumbe watatu wa Kamati Kuu kupinga nje ya kikao uamuzi wa chombo hicho na baadaye wajumbe wa Halmashauri Kuu kumwimbia mwenyekiti wao, Jakaya Kikwete wimbo wa kuonyesha wana imani na Edward Lowassa baada ya jina la mbunge huyo wa Monduli kuenguliwa na Kamati Kuu.
Jana, akitoa hotuba fupi baada ya kumalizika kwa sala ya Eid el Fitr kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam, Mwinyi alizungumza kwa mara ya kwanza hadharani kuhusu mchakato huo, akidokeza hali ilivyokuwa.
“Haikuwa kazi rahisi kwenye mchakato huu wa kumtafuta mgombea mmoja atakaye peperusha bendera ya CCM,” alisema Mwinyi lakini akawahi kuipoza kauli hiyo kwa kuelezea amani ilivyotawala mwishoni.
“Kama ni jahazi basi sasa tunashukuru limefika pwani salama.”
“Uchaguzi huu ni kwa ajili ya kuwapata viongozi wetu, tunataka viongozi bora wa kutuletea maendeleo, mapatano na wenye mahaba na wananchi.”
Akizungumza hadharani kwa mara ya kwanza baada ya mchakato huo wa kumtafuta mgombea wa urais kukamilika mjini Dodoma, Mzee Mwinyi alimshukuru Mungu kwa mchakato huo kuisha salama.
“Haikuwa kazi rahisi kwenye mchakato huu wa kumtafuta mgombea mmoja atakaye peperusha bendera ya CCM, kama ni jahazi basi sasa tunashukuru limefika pwani salama.
“Sasa, ninawaomba Watanzania kuwa watulivu katika kipindi hiki cha uchaguzi wa nchi tunaoufanyika kila baada ya miaka mitano,“ alisema Rais Mwinyi ambaye alikuwa mmoja ya wajumbe wa Baraza la Ushauri waliofanya kazi ya kutuliza wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM hadi kuafikiana kuendelea na mchakato wa kumpata mgombea urais.
Aliwasisitizia Watanzania kuacha tabia ya kupenda mno na kuacha kubaguana, akisema hakuna aliye bora na kuwataka kuzidisha mapenzi miongoni mwao na kusherehekea vyema Sikukuu ya Eid el Fitr. “Hakuna jambo lenye maana kama hili la kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye kutufikisha salama siku kama hii ya leo (jana) ambayo tunasherekea Sikukuu ya Eid,” alisema Mwinyi.
Awali Sheikh wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhad Mussa Salum aliwasisitizia wananchi umuhimu wa kusherekea sikukuu hiyo katika hali ya amani na utulivu.
Pia, aliwashauri wazazi na walezi kuwapeleka watoto wao sehemu zenye maadili ili washerehekee kama ambavyo Mwenyezi Mungu anapenda.

MWANANCHI
 Mwigizaji maarufu wa tamthilia ya Isidingo The Need, Jack Devnarain maarufu kwa jina la uigizaji la Rajesh Kumar, amefanikiwa kufika kilele cha Uhuru cha Mlima Kilimanjaro.
Rajesh, ambaye ni raia wa Afrika Kusini, pamoja na wenzake 36 walipanda mlima huo kuanzia Julai 14, kuadhimisha siku ya kuzaliwa kwa Hayati Nelson Mandela wa Afrika Kusini.
Mbali na kuadhimisha siku hiyo muhimu kwa Taifa la Afrika Kusini, pia walipanda kwa ajili ya kuchangisha fedha za kusaidia afya za watoto wa kike 272,000 wa nchi hiyo na Tanzania.
Mratibu wa Taasisi ya Mandela ya Trek4 Mandela nchini, Honest Minja alisema jana kwamba Kumar na wapanda mlima wenzake 31 kati ya 37 walifanikiwa kufika kileleni.
Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro (KINAPA), Erastus Lufunguloalisema kati ya watu 37 waliopanda mlima, 32 walifika kileleni na watano waliishia njiani.
Wageni 32 wa Trek4 Mandela wamefika kileleni akiwamo msanii wa Isidingo. Watatu waliishia kituo cha Kibo na wawili waliishia kati ya Kibo na kilelele cha Gilmans,” alisema.
Kundi hilo la wapanda mlima lilimjumuisha mpanda milima wa kimataifa Sibusiso Vilane ambaye ni Mwafrika wa kwanza kupanda mlima Everest ambao ni mrefu kuliko yote duniani.
Jana walitarajiwa kushuka hadi Kituo cha Horombo kilichopo urefu wa mita 3,720 na leo walitarajiwa kushuka hadi Mandara mita 2,700 na baadaye hadi lango kuu la Kinapa lililopo Marangu.
NIPASHE
Shughuli za usafirishaji jana zilisimama kwa zaidi ya saa mbili, baada ya msafara wa mgombea Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi(CCM), Dk. John Pombe Magufuli, kupita jijini hapa.
Licha ya kusimama kwa usafiri, msafara huo pia ulizuiwa kwa muda na wananchi katika eneo la Pasiansi, Kona ya Bwiru na Makongolo, wakishinikiza kusalimiana na mgombea huyo.
Magufuli ambaye aliongozana na viongozi mbalimbali wa CCM, serikali, madhehebu ya dini na wananchi wengine kutoka ndani na nje ya mkoa wa Mwanza alitua Uwanja wa Ndege saa 7:50 mchana.
Baadhi ya viongozi wa CCM taifa waliokuwa wameongozana na Dk. Magufuli ni pamoja na Katibu wa Siasa na Uenezi wa chama hicho, Nape Nnauye na Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Tanzania Bara, Rajabu Luhavi.
Kadhalika, Dk. Magufuli alikuwa amefuatana na mkewe, mama Janet Magufuli. Msafara wa Magufuli kuelekea  ofisi za CCM mkoani hapa uliondoka uwanja wa ndege Mwanza majira ya saa 8:30.
Akijitambulisha  mbele ya maelfu ya wakazi wa mkoa wa Mwanza  waliofurika nje ya ofisi ya CCM mkoani hapa, Dk. Magufuli  aliwapongeza wananchi kwa mapokezi yao makubwa, huku akiwataka Watanzania wote kuendelea kulinda  umoja wao kwa nguvu zao zote.
“Ninawashukuru sana kwa mapokezi yenu makubwa…lakini pia ninawaomba muulinde umoja wetu na tuendelee kushirikiana bila kujali itikadi za vyama wala rangi zetu,”Dk. Magufuli.
Aliahidi kuisimamia kwa kikamilifu Ilani ya CCM. Alisema atahakikisha wafanyabiashara ndogo ndogo hawanyanyaswi.
Awali akimkaribisha, Dk. Magufuli, Nnauye alisema CCM hakitasita kuwashughulikia wanachama wake ambao hulalamika  kwamba mchakato wa kuwapata mgombea urais kupitia chama hicho ulikiuka taratibu.
“Ninapenda kuwaambia kuwa mchakato wa kumpata mgombea urais ndani ya chama uliisha salama na tulimaliza salama ingawa kuna baadhi ya watu wanalalamika lalamika,” alisema.
Alisema wanaCCM hao watashughulikiwa na chama iwapo wataendelea na malalamiko hayo ambayo alisema hayana ukweli wowote.
“Wakiendelea tutawajibu, hasa wazee wetu.” alisema huku akishangiliwa.
Hii ni mara ya kwanza kwa Dk. Magufuli kufika Mwanza tangu achaguliwe na CCM kupeperusha bendera ya chama hicho kuwania nafasi ya urais kupitia uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu.
NIPASHE
Abiria zaidi ya 100 wanaokwenda mikoa ya Tabora na Kigoma wanaotumia usafiri wa treni wamekwama jijini Dar es Salaam kwa siku mbili baada ya Kampuni ya Reli nchini(TRL) kusitisha safari bila taarifa.
Abiria hao wengi wao wanawake na watoto, wamesema wanakabiliwa na hali mbaya ya kukosa chakula na huduma ya choo na kuhatarisha maisha yao.
Laurent Mayee mkazi wa Kigoma, alisema treni hiyo ilitakiwa kuanza safari juzi saa 11: 00 jioni lakini hadi jana saa 8 mchana hawajaondoka na hakuna kiongozi aliyejitokeza kutoa ufafanuzi.
Alisema  yeye na ndugu yake ambaye ni mgonjwa  walilipia Sh. 55,400 kila mmoja kwa behewa la daraja la pili, lakini tangu juzi asubuhi walipofika kituoni hapo wamejikuta wanasota kusubiri usafiri huo bila kuwa na uhakika wa lini wataondoka.
Mayee alisema uongozi wa TRL wamekuwa wakibadilisha ratiba kila wakati kupitia ubao wa matangazo.
Alisema ratiba ya kwanza iliyobadilishwa ilionyesha treni hiyo ingeanza safari saa 4:00 usiku, lakini ulipofika muda huo ilibandikwa ratiba nyingine ikionyesha safari hiyo imeahirishwa hadi jana saa 4:00 asubuhi.
Hata hivyo ratiba hiyo ilipanguliwa na kueleza safari ingeanza saa 11 jioni huku hakuna ufafanuzi wowote wa sababu za kuahirishwa kwake.
“Tangu tufike hapa jana (juzi) tumekuwa kama tupo gizani, hatujui lini treni itaondoka kitu kibaya zaidi tupo watu wengi tukiwa hatuna chakula, hatujui tutaishi vipi kwa siku zote tukiwa hapa,”  Mayee.
Abiria mwingine Hamisa Adamu anayesafiri kwenda  Kigoma, alieleza kwamba shida kubwa wanayokabiliana nayo ni kukosa sehemu ya kulala na vyoo vya kujisaidia hasa kwa  akina mama na watoto ambao hawana uwezo wa kulipia huduma hiyo.
Hamisa alisema hakuna anayepingana na kuwapo kwa tatizo, lakini ingetumika busara kwa viongozi kuongea na abiria hao kwa kuwaeleza tatizo pamoja na kusaidia mahitaji mbalimbali ya muhimu.
“Wewe fikiria mama atapata wapi pesa ya kulipia huduma ya choo Shilingi 300 ya kila anapohitaji yeye na mtoto wake, huku hajapata chakula wala maji tunaomba serikali kuingilia kati jambo hili haraka,” John Daniel.
Hata hivyo alipotafutwa Ofisa Habari wa kampuni hiyo Midladjy Maez kwa kutumia simu yake ya mkononi hakuweza kupatikana baada ya kuita bila kupokelewa.
Naibu Waziri wa Uchukuzi, Charles Tizeba, alipotakiwa kuzungumzia suala hilo, alisema hawezi kueleza chochote kwa sababu yupo katika msafara wa mgombea urais kupitia CCM, Dk. John Magufuli.
NIPASHE
Matatizo na manyanyaso yanayolalamikiwa na Watanzania yanadaiwa kutokana na mfumo mbovu wa serikali iliyopo madarakani inayotokana na Chama Cha Mapinduzi (CCM), kwa kushindwa kutetea maslahi ya wananchi wanyonge.
Tundu Lissu, aliwataka Watanzania kutomchagua mgombea aliyepitishwa na CCM kugombea urais Jonh Magufuli, maana hatakuwa na utendaji tofauti na viongozi waliomtangulia.
“Matatizo na changamoto zinazowakabili Watanzania zimetokana na mfumo mbaya wa CCM sio mtu, kwa hiyo wananchi wasimchague Magufuli wakidhani atatenda maajabu au mapya yatakayowafanya kuondokana na changamoto hizo,”  Lissu.
Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki, alisema Rais wa Awamu ya Nne,Jakaya Kikwete, alisifiwa sana wakati anachaguliwa lakini ameshindwa kutetea maslahi ya wananchi na badala yake umekuwapo mfumuko wa bei na kuongezeka kwa michango inayowaongezea maumivu wananchi.
“Wizi wa fedha za EPA, Richmond na Escrow, mbunge wenu (jimbo la Muleba Kaskazini) Charles Mwijage na Magufuli mbona hawakuwa na mtazamo tofauti na CCM ili muweze kuwaamini wapo tofauti na viongozi wengine wa chama hicho,”alihoji.
Alisema ili kudhihirisha CCM wanafanya maamuzi ya kuwaumiza wananchi makusudi, maamuzi yaliyofanyika bungeni ya kuletwa na kupitishwa kwa miswada ya dharura haikuwa mara ya kwanza maana miaka 18 iliyopita, serikali ya CCM ilileta muswada wa madini kwa dharura na sasa matokeo yake yanaonekana ya kuibwa kwa madini ambayo yangekuwa mkombozi kwa Watanzania.
Katika mkutano huo ambao pia ulitumika kumpigia debe mgombea ubunge katika jimbo la Muleba Kaskazini kwa tiketi ya Chadema, Ansbert Ngurumo, diwani wa kata ya Kamachumu, Danstan Mutagahywa, alitangaza rasmi kuhama CCM na kuhamia Chadema.
NIPASHE
Wimbi la watoto kutoroka majumbani limeibuka ambapo jumla ya wanafunzi wanne wameripotiwa kutoroka huku mmoja wa watoto hao akimwachia baba yake mzazi ujumbe kuwa ameamua kufanya hivyo baada ya kukerwa na kitendo cha walimu wake kumuadhibu bila kosa.
Wazazi wa wanafunzi hao waliofika kwenye ofisi za The Guardian zilizopo Mikocheni jijini Dar es Salaam, walieleza mazingira tofauti ya kutoweka kwa watoto wao akiwamo huyo aliyeacha ujumbe kwa baba yake.
Katika tukio la kwanza, mwanafunzi wa kidato cha tatu, Murtaza Petro (16) wa Shule ya Sekondari Mikwambe, ametoweka nyumbani na kumwachia baba yake ujumbe unaosomeka:
“Baba samahani mimi naondoka kwa sababu walimu wamenikasirisha wamenipiga mno bila kithibitisho wakasema nimekaa chimbo wakati sio kweli,’ baada ya maelezo hayo aliikunja na kuandika juu yake kuwa,
“Sio kwamba sipendi shule bali kitendo nilichofanyiwa.”
Baba mzazi wa mtoto huyo, Petro Murtaza, alisema mwanae alitoroka nyumbani Mei 16, mwaka huu na kwenda kusikojulikana.
Alisema siku moja nyuma Murtaza aliadhibiwa na walimu wake kwa kosa la kwenda kukata nywele kwenye eneo ambalo shule imezuia.
Petro amemuomba mtoto wake popote alipo arudi nyumbani ili aendelee na masomo yake na kuomba yeyote atakayemuona apige simu namba 0757 877588 au atoe taarifa kituo chochote cha polisi.
Katika tukio la pili, mwanafunzi wa darasa la nne, George Afumba (11) katika shule ya Msingi Atlas, jijini Dar es Salaam, naye ametoroka nyumbani mara baada ya kutumwa na mzazi wake akachukue nyanya gengeni.
Mama mzazi wa mtoto huyo Agnes Afumba alisema kuwa mtoto wake alitoroka wiki iliyopita na kwenda kusikojulikana.
Alisema mtoto huyo amekuwa na tabia za kutoroka nyumbani mara kwa mara na alipokamatwa hudai alikuwa kwenye michezo.
Alisema mara ya mwisho kutoroka ilikuwa ni mwezi wa Aprili ambaye alikaa mtaani kwa muda wa siku tatu na kukutwa kwenye baa ya Mango Garden akiangalia televisheni.
HABARILEO
Mahakama ya Wilaya ya Mpanda mkoani Katavi imemhukumu raia wa Burundi, Michael Lubandaya (18) kifungo cha miezi sita jela kwa kosa la kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura akiwa si raia wa Tanzania.
Raia huyo wa Burundi ambaye ni mkazi wa mjini Nyanza nchini Burundi anadaiwa kuingia na kuishi bila kibali ambapo alijiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura kwa jina la Abdallah Yusuph.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi, Dhahiri Kidavashari alisema mhamiaji huyo haramu anadaiwa kujiandikisha katika daftari la kudumu katika kituo kilichopo kijijini Kakese – Mbugani na kupatiwa kitambulisho cha mpiga kura chenye namba t1000- 4111-756-1.
“Katika uchunguzi wa awali mtuhumiwa alibainika kuwa ni mkazi wa Burundi na alijiandikisha huku akitambua kuwa si halali kufanya hivyo…baada ya upelelezi wa awali mtuhumiwa alifikishwa mahakamani na kuhukumiwa miezi sita,” alieleza Kidavashari.
Katika tukio lingine mkazi wa Chamazi, Dar es Salaam, Shaban Musa (38) amefikishwa katika mahakama ya wilaya ya Mpanda mkoani Katavi kwa kosa la kuingia ndani ya Kituo cha Polisi Mishamo na kuanza kupiga picha za mnato pasipo halali yoyote.
Kamanda Kidavashashri akisimulia mkasa huo alisema tukio hilo lilitokea Juni 29, mwaka huu saa kumi jioni katika kijiji cha Ifumbula wilayani Mpanda ambapo alikamatwa akiwa ameingia ndani ya eneo la kituo cha Polisi Mishamo na kuanza kupiga picha bila ruhusa.
“Ni kwamba, siku ya tukio mtuhumiwa alifika eneo hilo la kituo cha Polisi Mishamo na kuanza kupiga picha za mnato kwa kutumia kamera ya simu yake aina ya Huawei Model Y300 – 0100.
Hata hivyo mtuhumiwa hakuishia hapo aliamua kuelekea eneo lingine lililopo jirani na kituo ambalo kwa sasa linajengwa kituo kipya cha Polisi na kuendelea kupiga picha.
Wakati mtuhumiwa huyo akiendelea kupiga picha ndipo alipobainika na kukamatwa,” alieleza Kwa mujibu wa Kidavashari uchunguzi wa awali wa tukio hilo, mtuhumiwa alibainika kupiga picha ambazo zilileta mashaka kwani miongoni mwa picha alizokutwa nazo ni za viwanja muhimu vya michezo ambavyo kuna kuwa na mikusanyiko mikubwa ya watu, ofisi za kampuni ya wakulima(CAMCOS).
Picha zingine alizokutwa nazo ni pamoja na vibao vya kutambulisha maeneo mbalimbali ya Mishamo, picha za kituo cha Polisi mishamo ambacho kinafanya kazi na kinaendelea kujengwa na pia inadaiwa alipiga picha kituo cha afya Mishamo, kituo cha Umoja wa Mataifa cha Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) na makazi ya viongozi hao wa UNHCR.
JAMBOLEO
Migogoro ya ardhi wanayokabiliana nayo wakazi wa Kata ya Dodoma – Makulu, kwenye Manispaa ya Dodoma, imeelezwa kuwa itatumika kama kigezo kitakachotumiwa na wakazi hao, kuchagua viongozi katika ngazi za udiwani, ubunge na urais, unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu.
Hayo yalielezwa na baadhi ya wakazi wa Mitaa ya Kisasa, Medeli na Bwawani, wakiwa kwenye ofisi za CCM za Kata ya Dodoma Makulu walipomsindikiza mtia nia ya kuwakilisha chama hicho katika uchaguzi wa diwani wa kata hiyo, Lazaro Chihoma, aliporejesha fomu.
“Wakazi wa mitaa karibu yote ya kata hii, tumekubaliana Chifu wetu (Chihoma) awe kiongozi wa kisiasa wa kata yetu, kwa sababu kwa muda mfupi ambao amekuwa mwenyekiti wa serikali ya mtaa wa Bwawani, ametetea haki zetu dhidi ya waliotudhulumu ardhi,” Mchungaji wa Kanisa la Mitume, Yohana Mabene, alieleza.
Naye George Michael, mkazi wa Mtaa wa Medeli, alisema mtaa huo hauna mwenyekiti kufuatia wananchi kugoma katika uchaguzi wa viongozi wa serikali za mitaa nchini, kutokana na aliyekuwa mwenyekiti kwa zaidi ya miaka kumi, Stanley Chibwete, kudaiwa kuwa mgombea pekee aliyetakiwa kupigiwa kura.
Naye Chiloma ambaye pia ni chifu wa watu wa kabila la Kigogo, akizungumza mara baada ya kuwasilisha fomu za kuwania udiwani wa kata hiyo ambayo kwa sasa inaongozwa na diwani wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), alisema ameridhia ombi la wananchi wa kata hiyo na aliahidi kuwatumikia bila kuwaangusha.
Alisema endapo atachaguliwa kuwa diwani wa kata hiyo, ataendelea kutumia njia ya mazungumzo na maafikiano, kati yake kwa niaba ya wananchi anaowaongoza pamoja na mamlaka zinazohusika na usimamizi wa matumizi ya ardhi, kuhakikisha kila mwananchi anapata haki yake anayostahili.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA

DKT NCHIMBI ASHIRIKI MAZISHI YA ASKOFU.GACHUMA WA KANISA LA NLGCC

π™‚π˜Όπ™ˆπ™Šπ™‰π˜Ώπ™„ π™†π˜Όπ˜Ύπ™ƒπ™€π™•π˜Ό π™†π™„π˜½π™„π™‰π™‚π™’π˜Ό.