Urusi inasema kuwa msaidizi wa rubani wa ndege ya kijeshi iliyodunguliwa na Uturuki hapo jana ameokolewa na kurejeshwa katika kambi yao ya kijeshi iliyoo Syria.
Urusi inasema kuwa afisa huyo yuko katika hali njema katika kambi ya kijeshi ya Lattakia.
Wizara ya ulinzi nchini Urusi inasema kuwa rubani mwingine na mwanajeshi aliyeshiriki katika operesheni ya kwenda kuwaokoa marubani hao wa ndege iliyodunguliwa nao waliuawa.
Ubalozi wa Urusi na taarifa kutoka kwa serikali ya Syria zinasema kuwa rubani huyo aliokolewa na wanajeshi wa Syria na anarudishwa kwenye kambi ya jeshi la urusi eneo la Lattakia huko Syria.
Moscow inasema kuwa operesheni nchini Syria zitaendelea kuwakabili wapiganaji wa Islamic State na makundi mengine ya kijihadi.
Aidha Urusi imesema kuanzia leo ndege zinazoelekea kutekeleza operesheni za mashambulizi dhidi ya makundi ya kijihadi zitapewa ulinzi mkali na ndege za kivita.
Vilevile mitambo ya rada ya Urusi itatumika kuimarisha ulinzi wa angani katika maeneo ya mipakanai ya Syria.
Mitambo hiyo itawekwa katika kambi ya kijeshi ya Urusi iliyoko Lattakia.
Hayo yamejiri huku rais wa Marekani Barack Obama amemhakakishia mwenzake rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan kuwa nchi yake inaiunga mkono Uturuki katika jitihada za kulinda mipaka yake.
Hakikisho hilo la rais Obama linafwatia hatua ya Uturuki kuidungua ndege ya Urusi karibu na mpaka wa Syria.
Umoja wa mataifa na muungano wa kujihami ya nchi za Maghraibu NATO wamewataka Urusi na Uturuki kutuliza hasira zao.
Awali waandamanaji huko Moscow wameurushia ubalozi wa Uturuki mawe mayai na rangi wakionesha hasira zao kutokana na tukio la jana la kudunguliwa kwa ndege ya Urusi.
Uturuki ilidai ndege hiyo ilikiuka onyo la kutoingia katika anga yake kinyume cha sheria licha ya onyo isifanye hivyo.
Urusi imelitaja tukio hilo kama 'kudungwa kisu mgongoni'' na waandamanaji hao wanatika serikali yao ilipize kisasi...
Hata hivyo rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan anaonekana kujibu kauli ya rais Vladimir Putin ambaye amekuwa akimuunga mkono rais Asaad katika vita vya Syria.
" Hapa ukweli usemwe - kama unamuunga mkono mtu anaeyendeleza ugaidi katika taifa lake ...Na wewe unakiri kwa maneno na vitendo kwamba unauunga mwendelezo huo wa ghasia na vurugu basi hata nawe pia ni mkandamizaji ."
Hata hivyo licha ya matamshi hayo rais Erdogan amesisitiza kwamba anafanya kila jitihada kutuliza hali hiyo tete katika uhusiano wa nchi yake na Urusi akisistiza kuwa wana haki ya kulinda mipaka yao..
Comments