Na Daudi Manongi
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Mhe.John Pombe Magufuli ametoa wito kwa vyombo vya Habari nchini kuwa mbele
katika kusimamia Maadili na kuutangaza Utamaduni wa Mtanzania.
Rais Magufuli ameyasema hayo leo Ikulu Jijini
Dar es Salaam wakati wa Mahojiano ya mwaka na waandishi wa habari kwa mara ya
kwanza tangu aingie madaraka.
“Jukumu la kulinda Utamaduni na Maadili ya
mtanzania ni la kila mzalendo, mtanzania, mzazi na Wizara husika ipo kwa
ajili ya kusimamia jambo hili na vyombo vya habari mnatakiwa kuwa mstari wa
mbele kulisimamia kwa kuanzia katika vyombo vyenu vya Habari kutokana na kile
mnachoonyesha”Alisema Rais Magufuli.
Aidha Rais Magufuli amevitaka vyombo vya
Habari kuwa wazalendo katika kutengeneza vipindi vyenye mahadhi ya kitanzania
ili kuisaidia jamii kukua katika utamaduni wetu na kusaidia kujenga maadili
yaliyo bora.
Mbali na hayo Rais Magufuli amezungumzia
mafanikio mbalimbali yaliyopatikana katika kipindi chake cha mwaka mmoja toka
aingie madarakani ikiwemo kuongezeka kwa mapato kutoka bilioni 800 mpaka
makusanyo ya shilingi trilioni 1.5 kwa mwezi.
Pia amesema kuwa Bajeti ya mwaka 2016 ya
trilioni 29.5 iliyotenga asilimia 40 kwenye miradi ya maendeleo imekuwa yenye
mageuzi makubwa ukilinganisha na bajeti ya miradi hapo nyuma mabayo ilikuwa
asilimia 26 tu.
Pamoja na hayo Rais magufuli amesema kuwa
Serikali imeagiza ndege nyingine mbili zinategemewa kufika nchini mwanzoni mwa
mwaka 2018 ili kuboresha sekta ya utalii nchini.
Akizungumzia uundwaji wa serikali amesema
mategemeo yake katika serikali aliyoiunda imefanikiwa kwa kuwa Baraza
aliloliunda la watu wachache limekuwa la mafanikio makubwa na hili limetokana
na ushirikiano mkubwa wa mawaziri wake.
Rais Magufuli amevitaka vyombo vya habari
nchini kubadili mtazamo wao katika uandishi wao wa habari na kuandika habari
ambazo zina maslahi kwa Taifa na kuwahakikishia waandishi wa habari
kushirikiana nao kwa kuwa anatambua kazi nzuri wanayoifanya.
Comments