Manchester City "wataondolewa" kwenye michuano ya Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya iwapo hawatafunga katika mechi ya marudiano hatua ya 16 bora dhidi ya Monaco, meneja wao Pep Guardiola amesema.
City walitoka nyuma mara mbili na hatimaye wakafanikiwa kuwalaza viongozi hao wa ligi ya Ufaransa 5-3 mechi ya kusisimua iliyochezewa uwanja wa Etihad.
Mechi ya marudiano itachezwa 15 Machi.
"Tutasafiri Monaco na kufunga mabao mengi kadiri iwezekanavyo," Guardiola alisema baadaye.
"Hilo ndilo lengo langu. Ni vigumu kwetu kusonga tusipofunga bao."
Monaco waliongoza 2-1 na 3-2 kabla ya City kujikwamua na kupata ushindi.
Mechi hiyo inaongoza kwa kufungwa mabao mengi miongoni mwa mechi za mkondo wa kwanza hatua ya muondoano katika miaka 25 ya Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya.
Guardiola anatarajia mechi iwe wazi sana klabu hizo zitaapokutana tena.
Anahisi hiyo ndiyo njia bora zaidi ya kukabiliana na mashambulio makali ya Monaco ambao wamefunga mabao 76 mechi 26 za ligi Ufaransa msimu huu.
"Wanacheza kwa njia hiyo - watashambulia na kushambulia," alisema Guardiola.
"Tutahitaji kujilinda zaidi lakini tutapata nafasi. Nina uhakika kuhusu hilo.
"Je, nina furaha timu yangu ikifungua mchezo? Ndio. Sana."
Rekodi ya Pep Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya | ||
---|---|---|
Msimu | Klabu | Hatua Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya |
2008-09 | Barcelona | Fainali (wakawalaza Man Utd 2-0) |
2009-10 | Barcelona | Nusufainali (3-2, wakashindwa na Inter) |
2010-11 | Barcelona | Fainali (wakalaza Man Utd 3-1) |
2011-12 | Barcelona | Nusu fainali (3-2, wakalazwa na Chelsea) |
2013-14 | Bayern Munich | Nusu fainali (5-0 , wakalazwa na Atletico Madrid) |
2014-15 | Bayern Munich | Nusu fainali (5-3 , wakalazwa na Barcelona) |
2015-16 | Bayern Munich | Nusu fainali (2-2 sare na Atletico. Atletico wakasonga kwa magoli ya ugenini) |
Comments