Benjamin Sawe
Maelezo.
Bodi
ya mikopo ya Elimu ya Juu nchini imewataka wanaodaiwa na Bodi hiyo kurejesha
mikopo yao ili na wengine waweze kukopa badala ya kusubiri kuchukuliwa hatua.
Akiongea
katika kipindi cha Tunatekeleza kinachorushwa na Televisheni ya Taifa (TBC)
Mkurugenzi wa Bodi ya mikopo ya Elimu ya Juu Abdul Badru alisema tangu waanze
mfumo wa kuwabana wadaiwa kupitia waajiri wao kasi ya urejeshwaji mikopo
imeongezeka.
Alisema
pamoja na kuwabana pia wamekuwa wakitoa elimu kuhusu umuhimu wa kurejesha
mikopo hiyo pamoja na kutunga sheria ya kuwabana wasiolipa mikopo.
Awali
kabla ya kuwekwa kwa msukumo katika kudai mikopo hiyo urejeshwaji ulikuwa
wastani wa shilingi bilioni 5 mpaka 6 kwa mwezi lakini kwa sasa wanapata
marejesho ya mikopo zaidi ya Bilioni 10. Bw.
Badru alisema hivi sasa wameboresha mfumo wa utoaji mikopo kwa kuziba mianya ya
wanafunzi hewa pamoja na wale wasiokuwa na sifa ambao wamekuwa wakipeleka
vielelezo vya uongo.
Alisema
licha ya kupitishwa kwa orodha ya wanafunzi wanaostahili mikopo uhakiki umekuwa
ukifanyika kila baada ya miezi mitatu ambapo maofisa wa bodi hiyo huenda vyuoni
ili kujiridhisha kama wanafunzi waliolengwa kwenye mikopo hiyo wapo.
“Kwa
mfano mwaka jana wanafunzi elfu tatu miongoni mwa walioomba mikopo kwa madai ya
kufiwa na wazazi waliwasilisha vyeti vya Vifo vya wazazi wao ambavyo baada ya
kupelekwa RITA walishindwa kuvitambua”Alisema BADRU.
Alisema
mwanafunzi anayekosa mkopo kama anavyo vigezo vyote vinavyotakiwa hutakiwa
kukata rufaa ili ufanyike upitiaji upya wa nyaraka zake.
Kwa
mwaka wa fedha 2016/2017 jumla ya shilingi Bilioni 483 zimetengwa kwaajili ya
kuwakopesha wanafunzi 120,000 kutoka vyuo tofauti nchini.
Comments