Bingwa wa zamani wa Olimpiki katika mbio za 1500m Mkenya Asbel Kiprop amesema atathibitisha kwamba yeye ni "mwanariadha msafi" baada ya taarifa kuibuka kwamba aligunduliwa akiwa ametumia dawa zilizoharamishwa michezoni.
Mwanariadha huyo wa miaka 28 ambaye ni bingwa wa dunia mara tatu alipatikana akiwa ametumia dawa za kuimarisha damu aina ya EPO.
Aligunduliwa baada ya kufanyiwa vipimo wakati akiwa hashiriki mashindano.
Kiprop alimaliza wa pili Michezo ya Olimpiki ya mwaka 2008 jijini Beijing lakini akakabidhiwa dhahabu baada ya mshindi Rashid Ramzi kutoka Bahrain kubainika kwamba alikuwa ametumia dawa zilizoharamishwa.
Kupitia taarifa, Kiprop amesema hawezi kuharibu maisha yake ya uanariadha kwa kutumia dawa zilizoharamishwa.
"Nimekuwa kwenye mstari wa mbele katika vita dhidi ya matumizi ya dawa za kuongeza nguvu mwilini katika michezo Kenya - na nina imani na naunga mkono vita hivi," alisema Kiprop ambaye anashikilia nafasi ya tano ya muda bora zaidi katika historia kwenye mbio za 1500m.
"Siwezi kutaka kuharibu mambo ambayo nimeyafanyioa kazi tangu niliopokimbia mbio zangu za kwanza za kimataifa 2007. Ninatumai kwamba ninaweza kuthibitisha kwamba mimi ni mwanariadha 'msafi' kwa njia yoyote ile inayowezekana."
Asbel Kiprop ndiye Mkenya wa karibuni zaidi kujipata katika sakata la kutumia dawa zilizoharamishwa.
Mabingwa wengine waliopatikana na kosa hilo ni pamoja na Jemima Sumgong ambaye alipigwa marufuku ya kutoshiriki shindano lolote kwa muda wa miaka minne.
Bingwa wa zamani wa Boston na Chicago Marathon Rita Jeptoo alipatikana na makosa ya kutumia EPO mwaka 2014 na akapigwa marufuku ya miaka minne pia.
Wanariadha zaidi ya 40 kutoka Kenya wamepatikana na kosa la kutumia dawa za kutitimua misuli katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.
Comments