Sheria ya uhalifu wa kimitandao Kenya: Kenyatta aidhinisha sheria inayotoa adhabu ya dola 50,000 kwa habari feki
Rais wa Kenya Uhuru
Kenyatta ameidhinisha Mswada wa Sheria za Uhalifu wa Kompyuta na
Mtandaoni wa 2018 kuwa Sheria, hatua itakayotoa adhabu kali kwa
watakaopatikana na makossa ya mtandaoni.
Sheria hiyo inatoa adhabu ya faini ya Sh5 milioni (dola 50,000
za Marekani) au kifungo cha miaka miwili jela, au adhabu zote mbili, kwa
atakayepatikana na kosa la uenezaji wa habari za uzushi.Mtu atakayepatikana na kosa la kueneza taarifa ambazo zinaweza kuzua taharuki au kuzua vurugu atafungwa jela zaidi ya miaka kumi.
Sheria hiyo inatarajiwa kuathiri utendakazi wa wanahabari, vyombo vya habari, watumiaji wa mitandao ya kijamii, wanablogu na watu wengine wanaotumia kompyuta na mitandao.
Lakini je ni kweli sheria hiyo mpya itakandamiza uhuru wa kujieleza?
Wakati wa maadhimisho ya siku ya uhuru wa wanahabari mapema mwezi huu, mwenyekiti wa Chama cha Wahariri Kenya Bw Churchill Otieno alikuwa amesema sheria hiyo inaweza kutumiwa kuminya uhuru wa wanahabari.Alieleza kuwa kifungu kinachozungumzia uenezaji wa habari za uzushi au uongo kinaweza kutumiwa vibaya na maafisa wa dola.
Kiongozi wa zamani wa Chama cha Wanasheria Kenya Apollo Mboya amenukuliwa na vyombo vya habari akisema kifungu hicho kinaweza kuwapa watawala 'uhuru' wa kukandamiza vyombo vya habari.
Shirika la kimataifa la kutetea uhuru wa wanahabari Committee to Protect Journalists (CPJ) nalo lilikuwa limemhimiza Rais Kenyatta kutoidhinisha mswada huo kuwa sharia.
Makundi ya kueteta haki za binaadamu wameishutumu sheria hiyo na kuitaja kuwa ya hatari.
Shirika la Article 19 East Africa, linataja makosa kadhaa yalio mapana ambayo yana adhabu kali zinazoweza mwishowe kuzuia uhuru wa kujieleza katika mitandao Kenya.
Comments