Leo jijini Dar es Salaam nimeungana na viongozi wengine wa Afrika kufungua Mkutano Mkuu wa Wanahisa wa Taasisi ya Africa50 na Jukwaa la Miundombinu Afrika, ambapo Tanzania imepata heshima ya kuwa mwenyeji. Jukwaa hilo, linaloadhimisha miaka 10 tangu kuanzishwa kwake, limekuwa sehemu muhimu ya kuunganisha mitaji, miradi na wataalamu ili kuharakisha maendeleo ya miundombinu barani Afrika.
Katika mkutano huo nimeeleza kuwa, Tanzania inashirikiana kwa karibu na sekta binafsi katika kuimarisha miundombinu, ikiwemo barabara, reli, bandari na viwanja vya ndege. Hatua hii inachochea ukuaji endelevu wa uchumi kwa kupunguza gharama za usafirishaji, kukuza biashara, kuvutia uwekezaji, kutoa ajira na kuifanya nchi yetu kuwa kitovu cha usafirishaji.
Kutokana na mabadiliko ya kiuchumi, kisiasa na kimazingira duniani, nimesisitiza umuhimu wa Afrika kuimarisha miundombinu inayohimili mabadiliko hayo na kuunganisha nchi zetu ili kuendelea kukuza biashara, uwekezaji na uongezaji thamani wa rasilimali zetu.
Comments