TAMISEMI HAIVUNJI SHERIA KUANDAA KANUNI ZA UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA

OR-TAMISEMI


WADAU wa uchaguzi wamesisitiza kuwa hatua ya Ofisi ya Rais-TAMISEMI kuandaa kanuni za uchaguzi wa serikali za mitaa haivunji sheria yoyote.

Akichangia utoaji maoni wa kanuni za uchaguzi wa serikali za mitaa, Mkurugenzi Mtendaji wa shirika lisilo la kiserikali la Women in Social Entrepreneurship (WISE), Astronaut Bagile amesema wananchi wanapaswa kuelewa kuwa hakuna sheria yoyote imevunjwa katika mchakato wa uchaguzi wa serikali za mitaa.

“Niwatoe hofu watanzania kuwa huu uchaguzi si kwamba unavunja sheria iliyopitishwa na bunge, leo tunazungumzia uchaguzi wa serikali za mitaa na hakuna mahali ilipokesewa na sana sana unaakisi adhima ya Serikali ya kuhakikisha kwamba demokrasia inarudi kwa wananchi kwasababu Serikali za mitaa ndipo wananchi wanapoishi na wanategemea huduma mbalimbali ziletwe kwao kupitia serikali yao.”

Dk.Bagile alisema ukatili wa kijinsi umekuwa kikwazo kwa wanawake kushiriki kwenye chaguzi za serikali za mitaa na kusisitiza kuwa kanuni hizo zinaenda kuwakaba wale wote wanajiingiza katika kutoa kejeli matusi na vitisho kwa wanawake ambao wanajitokeza kuwania nafasi za uongozi.

Akifungua kikoa hicho cha kupokea maoni ya rasimu ya kanuni za uchaguzi wa serikali za mitaa leo jijini Dodoma, Naibu Waziri wa Tamisemi, Dk Festo Dugange amesema sheria ya Serikali za Mitaa inampa dhamana Waziri mwenye mamlaka za Serikali za mitaa kuandaa kanuni za uchaguzi wa Serikali za Mitaa na kusimamia uchaguzi huo.

“Na kanuni hizo zitawasilishwa kwenu kwa ajili ya kupata maoni. Nimeona nianze kwa kutoa ufafanuzi huu ambao mara nyingi maeneo mbalimbali tumekuwa tukipata hoja za wadau kuwa ni namna gani mamlaka hii inahusika na uchaguzi wa Serikali za Mitaa.”

Dk. Dugange amesema maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan ametaka uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa Mwaka 2024, kuwa huru na haki na kwamba rasimu hiyo imezingatia maoni ya wadau.

Naye Shehe Mkuu wa Jumuiya ya Shiha (TIC) Tanzania, Hemed Jalala alipongeza hatua ya Serikali ya kuwashirikisha viongozi wa dini na watu tofauti tofauti katika kutoa maoni na kusema hatua hiyo inawapa nguvu viongozi wa dini.

“Nipongeze serikali kwa kutukusanya kutoa maoni viongozi wadini ambao ni wadau muhimu katika kuhubiri amani, upendo na wa kutawaka watanzania wavumiliane na wakae vizuri,”

Alisema hatua ya Ofisi ya Rais-TAMISEMI kuwakutanisha viongozi wa dini na kutoka maeneo tofauti tofauti ni ishara ya nia njema ya Rais Samia na wizara ya kutenda haki na kuimarisha demokrasia ndani ya Tanzania.

Alisema kitendo hicho pia kinaonesha ujasiri wa Rais Samia na kuwapa nguvu viongozi wa dini wanapokutana na waamini wao siku za jumapili na ijumaa kuendelea kuhubiri umuhimu wa kukaa kwa amani, mshikamano, kuvumiliana.

Naye Askofu Mkuu wa Kanisa la Elim Pentekoste Tanzania, Peter Konki aliishauri serikali kuongeza wigo wa kupokea maoni kuhusu maboresho ya rasimu ya kanuni hizo.

“Unapowapa watu uhuru wa kuweka mawazo yao katika kuweka Serikali madarakani kunajenga imani kwa wananchi na kuwa karibu na serikali na haki ya kuitetea serikali na kuwa sehemu ya serikali.”

Kwa upande wa Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Tanzania Padri Charles Kitima alishauri kuwepo uwazi wakati wa wagombea wanaporejesha fomu ili kuondoa manunguniko pale mtu anapoenguliwa kushiriki uchaguzi.

Naye. Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Kivulini la jijini Mwanza, Yassin Ally alishauri kanuni hizo kutoa uwiano sawa kwa wanawake kuongombea nafasi za uongozi katika mamalaka za serikali za mitaa.

Akitoa maoni, Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki Tanzania (TEC), Padri Charles Kitima alitaka kuwepo kwa uwazi wakati wa uteuzi wa wagombea kwenye uchaguzi huo.

“Inapotokea kuwa kuna mgombea mmoja tu, mazingira yaangaliwe ili isije ikawa mtu amejenga mazingira ya kubaki pekee yake.”

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Maridhiano na Amani, Askofu Israel Maasa alishauri viongozi wa dini kuwa sehemu ya waaangalizi wa uchaguzi huo, jambo ambalo litasaidia viongozi hao kuweza kujibu kelele ambazo zinaweza kujitokeza mara baada ya uchaguzi.

Pia alishauri Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kujizatiti kiasi cha kutokutumiwa na wagombea na kuhakikisha wanafanyia uchunguzi wa kina tuhuma za wagombea kabla ya kuwakamata.

Mwakilishi wa Shirika lisilo la Kiserikali linalojishughukisha na vijana la Restless Development, Badru Rajabu alisema uhitaji wa vitambulisho kwa mpigakura unaweza kusababisha wengi wa watu kutopiga kura kwenye uchaguzi huo na kushauri watendaji wanaweza kuwaandikia barua za utambulisho.

Naye Mtaalamu wa Usawa wa Kijinsia wa UN Women Tanzania Stella Manda alipendekeza kuainishwa ni makosa gani ya unyanyasaji wa jinsia yanayokatazwa kupitia kanuni hizo.

Kwa upande wake Mwanasheria wa Ofisi ya Rais - Tamisemi Kadete Mihayo alisema taasisi zitakazotoa elimu ya uraia zitatoa kwa gharama zao na pia kutakuwa na waangalizi wa ndani wa uchaguzi ambao wataomba kufanya hivyo.

Pia alisema hakutakuwa na mgombea kupita bila kupingwa.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

RAS KILIMANJARO NA DEREVA WAFARIKI KWA AJALI, MKUU WA MKOA ADHIBITISHA

BALOZI NCHIMBI MSIBANI KWA TIXON NZUNDA

JKCI YASHIRIKI KAMPENI YA AFYA CHECK KUTOA HUDUMA ZA MATIBABU YA MOYO

BALOZI NCHIMBI AONGOZA MAPOKEZI YA KATIBU MKUU, MGOMBEA URAIS WA FRELIMO

CRDB BUNGE BONANZA LAFANA DODOMA

MBUNGE MBOGO AWAALIKA BUNGENI VIONGOZI UWT KATAVI

BALOZI NCHIMBI AWAONGOZA WAOMBOLEZAJI MAZISHI YA NZUNDA SONGWE

DKT NCHIMBI AUNGURUMA KILIMANJARO

WAZIRI WA FEDHA AWASILISHA BAJETI YA 2024/2025