TBS YATAJA MAFANIKIO LUKUKI AWAMU YA RAIS SAMIA

 

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Dkt. Ashura Katunzi, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio na mwelekeo wa shirika hilo katika kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita leo Machi 18, 2025, katika Ofisi za Idara ya Habari - MAELEZO, jijini Dodoma.


1.    MAFANIKIO NA MUELEKEO WA TBS KATIKA MIAKA MINNE YA SERIKALI YA AWAMU YA SITA

Kipindi cha miaka minne (2021-2024) ya Serikali ya awamu ya Sita, kimekuwa cha mafanikio makubwa kwa Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika utekelezaji wa majukumu yake. Mafanikio hayo yameendelea kutimiza azma ya Shirika katika masuala mbalimbali ili kutimiza matamanio ya wadau na Taifa kwa ujumla kama ifuatavyo:

 

a)   Kusogeza Huduma Karibu na Wateja

 

Katika kutekeleza azma ya Serikali kuhakikisha wananchi wanapata huduma kwa ukaribu na kupunguza gharama, Shirika limeanza ujenzi wa maabara katika mikoa ya kimkakati ya Dodoma na Mwanza.

 

Kwa upande wa Dodoma, maabara zitakazojengwa zitahudumia mikoa mitatu ya Kanda ya Kati ambayo ni Dodoma, Singida na Tabora pamoja na mikoa mingine ya karibu. Aidha, maabara za Mwanza zinatarajiwa kuhudumia mikoa sita, ambayo ni Mwanza, Kagera, Mara, Geita, Shinyanga na Simiyu. Pia Shirika limeshapata Mshauri Mwelekezi (Consultant) wa kuchora michoro ya jengo pamoja na kusimamia ujenzi wa maabara na ofisi jijini Arusha. Hatua hiyo ya ujenzi wa maabara itasaidia kusogeza huduma karibu na wananchi na kuongeza ufanisi katika utoaji wa majibu ya vipimo vya sampuli.

Shirika limetenga kiasi cha TZS bilioni 2.7 kwa ajili ya kuimarisha ofisi saba za kanda (Arusha, Mwanza, Mtwara, Dar es Salaam, Dodoma, Kigoma na Mbeya) pamoja na ofisi za mipakani (Tunduma, Kasumulo, Horohoro, Holili, Tarakea, Namanga, Bandari ya Mwanza, Uwanja wa Ndege wa Mwanza, Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro, Sirari, Kabanga, Rusumo, Mutukula, Bandari ya Bagamoyo, bandari ya Mbweni, bandari ya Dar es Salaam, Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Kambarage Nyerere – Dar es Salaam na Bandari ya Tanga) kwa kuongeza wafanyakazi na vitendea kazi kwa ajili ya kutoa huduma kwa wakati na kuimarisha zoezi la ukaguzi wa mara kwa mara sokoni ili kupunguza bidhaa hafifu sokoni na hatimaye kuhakikisha wananchi wanapata bidhaa bora na salama.

 

a)   Kuwezesha Biashara

 

Shirika lina Kamati za Kitaalam (Technical Commitees) za Uandaaji Viwango 115 katika sekta ya chakula, kemikali, uhandisi mitambo, uhandisi umeme, uhandisi ujenzi, nguo na ngozi, madini na mitambo ya uchimbaji madini, mazingira na mtambuka (general tecniques).  Katika mchakato wa kuandaa viwango Kamati hizo zinashirikisha wadau mbalimbali ikiwemo vyuo vikuu, taasisi za utafiti, wafanyabiashara, wazalishaji, vyama vya walaji, vyama na bodi za wataalam, taasisi za udhibiti na watunga sera. Kwa kipindi cha miaka minne Shirika limefanikiwa kuandaa viwango 1,823 vya sekta mbalimbali kwa kuzingatia mahitaji ya soko ambavyo vitasaidia wafanyabiashara, wajasiriamali na watoa huduma kuzalisha bidhaa bora zenye kukidhi matakwa ya viwango, hivyo kuwawezesha kufanya biashara ndani na nje ya nchi, hatua ambayo italeta tija na kuchochea ukuaji wa uchumi.

 

Aidha, jumla ya vyeti na leseni za ubora 2,402 vimetolewa kwa wazalishaji, miongoni mwao wakiwemo wajasiriamali wadogo 1,066. Serikali kupitia TBS imekuwa ikitenga zaidi ya sh. milioni 350 kila mwaka kwa madhumuni ya kuhudumia wajasiriamali wadogo bila ya malipo yoyote. Leseni hizi zimesaidia wazalishaji kuweza kuzalisha bidhaa bora, ikiwa ni pamoja na bidhaa zao kuweza kuaminika sokoni na pia kufanya biashara nje ya mipaka ya Tanzania, hivyo kuchochea kasi ya ukuaji wa uchumi wa Taifa.

 

Katika kipindi cha miaka minne, Shirika limeendelea na huduma za usajili wa maeneo ya uzalishaji, uuzaji, usambazaji na uhifadhi wa chakula na vipodozi kwa lengo la kuhakiki ubora na usalama wa maeneo hayo ili kuendelea kulinda afya za walaji ambapo jumla ya maeneo 31,592 yalisajiliwa.

 

Pia, katika kuimarisha ukaguzi wa bidhaa mbalimbali zinazoingia nchini kutoka nchi za nje, TBS huhakiki ubora wa bidhaa na magari yaliyotumika kabla ya kusafirishwa kuja nchini ambapo kwa kipindi cha miaka minne, jumla ya shehena za bidhaa 18,588 zilikaguliwa, sanjari na magari 162,160. Bidhaa hizi 

zinakaguliwa kwa lengo la kuiepusha Tanzania kuwa jalala la bidhaa duni pamoja na kulinda afya, usalama na mazingira ya watumiaji.

 

Kwa upande wa mafunzo, TBS imeweza kutoa mafunzo kwa jumla ya wadau 5,052 wakiwemo wazalishaji wa bidhaa za viwandani na wasindikaji. Mafunzo hayo yalihusu dhana nzima ya viwango na ubora ambayo yatawawezesha kuzalisha bidhaa zinazokidhi matakwa ya viwango na yamewawezesha kupata uelewa mpana kwenye masuala ya udhibiti ubora, hivyo kuwaandaa kuhimili ushindani wa masoko ya ndani, kikanda na kimataifa.  Pia kupitia Mradi wa Qualitan TBS na SIDO mwaka 2024 waliwezeshwa kutoa mafunzo kwa wazalishaji wa bidhaa za chakula 1000 katika mikoa 10 (Dar es Salaam, Singida, Mwanza, Geita, Kagera, Kigoma, Shinyanga, Tanga, Ruvuma na Kilimanjaro)

 

Vilevile, TBS imeendelea kutoa elimu kwa umma kupitia njia mbalimbali ili kukuza uelewa juu ya masuala ya viwango na udhibiti ubora. Njia hizo ni pamoja na kushiriki katika makongamano, maonesho, warsha na semina; kuandaa mikutano na wadau wa masuala ya viwango, kutoa mafunzo mbalimbali kuhusu masuala ya ubora na usalama; na kuendesha kampeni za elimu kwa umma katika ngazi za wilaya. Aidha, elimu imekuwa ikitolewa kupitia vyombo vya habari zikiwemo redio jamii, redio za kitaifa, runinga, magazeti, mitandao ya kijamii, matangazo, majarida na vipeperushi.

 

 

a)   Kuongeza Ufanisi wa Maabara

TBS ina jumla ya maabara 12 na zote zimeweza kupata ithibati za umahiri, ambapo maabara hizo zimehakikiwa na kupatiwa vyeti vya ithibati ya umahiri wa kimataifa. Hatua hiyo inamaanisha kuwa majibu ya sampuli kutoka katika maabara hizo yanaaminika kokote duniani na hivyo kurahisisha biashara ndani na nje ya mipaka ya nchi yetu. Katika kipindi hicho TBS imeweza kupima sampuli zaidi ya ya 118,059 na kufanyia ugezi vifaa 36,808 ambapo suala hili litasaidia kuhakikisha katika soko kunakuwa na bidhaa zenye ubora.

 

Maabara za TBS zina mashine za kisasa (state-of -art-equipment) zinazopelekea kupata majibu kwa wakati na sahihi, pamoja na mashine nyingi zilizopo katika maabara hizo, kuna mashine za kipekee kama ifuatavyo;

i)     Mashine ya hydrostatic pressure test ya kupima mabomba ya maji na yenye uwezo wa kupima mabomba yenye kipenyo cha milimita 12 sawa na inch 0.5 hadi milimita 800 sawa na inchi 32. Mashine hii ina uwezo pia wa kupima sampuli 120 kwa wakati mmoja na kati ya nchi 54 za Barani Afrika inapatikana katika nchi tano tu ikiwemo Tanzania;

ii)    Mashine ya automatic conductor resistance tester ya kupimia waya (cables) za umeme za aina zote zenye kipenyo hadi kufikia milimita 40 sawa na milimita za mraba1200. Mashine hii ni ya kipekee kwa kuwa ni ya kidigitali na ina uwezo wa kupima na kutoa majibu kwa haraka;i)     Mashine ya solar simulator ambayo katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati inapatikana Tanzania pekee katika ofisi zetu za TBS. Mashine hii inauwezo wa kupima solar panels za aina zote bila kutegemea uwepo wa jua.

 

a)   Kuimarisha Mifumo ya TEHAMA

 

Shirika linatumia mifumo ya TEHAMA katika utoaji wa huduma zake mbalimbali kama vile leseni ya ubora, ukaguzi wa shehena zinazotoka nje ya nchi na usajili wa bidhaa za chakula na vipodozi, majengo, maeneo ya uzalishaji, uuzaji, vyombo vya usambazaji wa bidhaa za chakula na vipodozi. Mifumo hiyo ni OAS na i-SQMT. Aidha, Shirika limeboresha huduma zake kwa wafanyabiashara wanaoingiza bidhaa nchini kwa kuunganisha mfumo wake unaoitwa Online Application System na mfumo wa Dirisha Moja la Huduma (Tanzania electronic Single Window System – TeSWS) ambapo mfanyabiashara anatuma maombi na anapata huduma za taasisi zote na kibali kupitia mfumo huo.

 

 

 

b)  Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia

TBS inatambua na kusifu juhudi za Serikali katika kuboresha upatikanaji wa nishati safi, kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi, na kutunza mazingira huku ikiokoa maisha kupitia suluhisho endelevu la upatikanaji wa nishati safi ya kupikia.TBS ina jukumu muhimu kama taasisi ya viwango nchini katika kuhakikisha utekelezaji wa viwango vya kitaifa vya nishati unasaidia kufanikisha malengo hayo.TBS inashirikiana na 

washirika wa maendeleo na Wizara ya Nishati kuandaa viwango vya ufanisi wa nishati kwa vifaa vya umeme vya majumbani. Vilevile vifaa vya Maabara vya kisasa vinaendelea kununuliwa kwa ajili ya kuhakikisha vifaa vinavyoingia sokoni vinakidhi viwango vilivyowekwa kabla ya kuwafikia watumiaji. Hatua hii inalenga kupunguza uzalishaji wa gesi joto, kupunguza upotevu wa nishati, na hivyo kupunguza gharama kwa watumiaji.

 

a)   Tuzo na Umahiri

 

Mnamo mwaka 2023, TBS ilipata mafanikio makubwa kwa kushinda Tuzo ya kuwa Mdhibiti Bora Barani Afrika kwa Mwaka 2023. Tuzo hii inaonesha dhamira ya TBS katika utendaji bora na mchango wake chanya katika kukuza viwango na kudhibiti ubora.

 

Vilevile, TBS imekuwa taasisi ya kwanza katika Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) kupata ithibati (accreditation) ya mifumo ya udhibiti ubora wa bidhaa (Product Certification) ya kimataifa katika wigo mpana (wide scope) ndani ya muda mfupi na ni ya taasisi ya tatu kupata ithibati hiyo iliyotolewa na SADCAS Septemba, 2024 hivyo kufanya mifumo hiyo kutambulika kimataifa.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

RAIS TRUMP ARARUANA NA RAIS WA UKRAINE

MWABUKUSI ATOA NENO SIMBA KUSUSIA DERBY DHIDI YA YANGA

SERIKALI YALIKUBALI OMBI LA DIAMOND

HOSPITALI YA MUHIMBILI YAANZISHA HUDUMA YA KISASA YA KUZIBA MAPENGO

MWANAMKE ALIYEVUNJA REKODI KWA KUZAA WATOTO 69

ARAJIGA AULA KOMBE LA DUNIA