TUMEANDIKA HISTORIA KUBWA, UZINDUZI WA MAKAO MAKUU YA ULINZI WA TAIFA - RAIS SAMIA

 Na Richard Mwaikenda, Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema kuwa Serikali yake ya Awamu ya Sita imeandika historia  nyingine kubwa kwa Taifa  kwa kuzindua Makao Makuu ya kwanza ya Ulinzi wa Taifa (MMUT) mkoani Dodoma na kwamba hatua hiyo  imekamilisha maono ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere ya mwaka 1964 wakati Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) lilipoundwa.

 

"Leo tumeandika historia nyingine kubwa kwa Taifa letu kwa kuzindua Makao Makuu ya kwanza ya Ulinzi wa Taifa eneo la Kikombo mkoani Dodoma. Hatua hii imekamilisha maono ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere ya mwaka 1964 wakati Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) lilipoundwa."

 

"Majengo haya ambayo tumeyajenga kwa fedha na wataalamu wa ndani ni uthibitisho wa ukomavu wa Taifa letu katika kupanga, kuamua na kutekeleza kwa ufanisi miradi mikubwa. Kuziweka pamoja ofisi za JWTZ na Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kutaongeza tija na ufanisi wa kazi, na ni kielelezo cha dhamira yetu ya kujenga taasisi imara za kulinda uhuru, mipaka, rasilimali na watu wetu," amesema Rais Samia huku akishangiliwa.

 

"Mafanikio ya mipango tuliyojiwekea yanategemea sana uwepo wa amani na utulivu. Hivyo, wito wangu kwetu sote ni kuendelea kuimarisha ulinzi, usalama, umoja na mshikamano wa nchi yetu." Amesema Rais Samia.

 

Naye Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa JKT ,Dkt .Rhimo  Nyansaho amesema ujenzi wa makao makuu hayo unaonesha dhamira ya wazi ya serikali katika kuimarisha suala la ulinzi na usalama nchini.

Amesema jengo hilo la kisasa litaongeza ufanisi katika uratibu wa shughuli za kiulinzi na kutoa mazingira bora ya utendaji kazi kwa maafisa na askari.

“Uwepo wa makao makuu ya kudumu ni hatua muhimu katika kujenga taasisi imara, zenye mifumo madhubuti ya kiutendaji na mawasiliano, jambo litakalosaidia kukabiliana na changamoto za kiusalama zinazoibuka katika ulimwengu wa sasa.”amesema Dkt.Nyansaho.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Katibu Mkuu Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Faraji Mnyepe amesema serikali imeandika historia mpya kwa kuwa na makao makuu ya kudumu ya ulinzi wa taifa.

Amesema zaidi ya shilingi bilioni 121 zimetumika katika kufanikisha ujenzi huo wa awamu ya kwanza ambao umetekelezwa na wataalamu wa ndani ya jeshi hilo.

“Matumizi ya wataalamu wa ndani yamepunguza gharama na kuongeza uzoefu kwa wanajeshi katika sekta ya ujenzi na usimamizi wa miradi mikubwa ya kimkakati. ameongeza kuwa mradi huo umezingatia viwango vya kisasa vya ubora na usalama.”amesema Dkt.Mnyepe.

Kwa upande wa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi  Tanzania, Jenerali Jacob John Mkunda amesema jengo hilo ni sehemu ya kurahisisha utendaji kazi na kuchochea uimarikaji wa ulinzi na usalama wa taifa. amesema makao makuu hayo yatawezesha upangaji na utekelezaji wa mikakati ya kiulinzi kufanyika kwa haraka na ufanisi zaidi.

Aidha amewahimiza wanajeshi kuendelea kufanya kazi kwa nidhamu, uadilifu na uzalendo, wakitambua kuwa jukumu lao ni kulinda uhuru, umoja na mshikamano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Taswira ya Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo Mkoani Dodoma mara baada ya kuzinduliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, tarehe 24 Februari, 2026.



Rais na Amiri Jeshi Mkuu, Dkt. Samia Suluhu Hassan akipiga light pistol juu kuashiria uzinduzi wa jengo la Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa (MMUT), Kikombo Mkoani Dodoma tarehe 24 Februari, 2026.
Rais  na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimkabidhi bendera Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania, Jenerali Jacob John Mkunda.


Akikabidhi ufunguo wa jengo hilo kwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Rhimo S. Nyansaho.
Akipigiwa wimbo wa Taifa na baadaye kupigwa mizinga.
Akikagua gwaride la vikosi vya ulinzi.


Baadhi ya waambata wa majeshi wanaoziwakilisha nchi zao nchini.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Maafisa Askari, Watumishi wa umma na wageni mbalimbali waliohudhuria uzinduzi

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

Wasifu wa Kizza Besigye

KILA MWANAMKE ANAPASWA KUFAHAMU HII...

MBUNGE DKT. MAJULE ATOA MSAADA WA VYAKULA, VYANDARUA 100 SHULE YA VIZIWI DODOMA

Kizza Besigye ‘akamatwa’ tena Uganda

MAMBO MADOGO YANAYOVUTIA KWA MPENZI WAKO

DKT. MAJULE AKABIDHIWA CHETI CHA SHUKRANI UWT DODOMA KUFANIKISHA USHINDI WA CCM 2025

30 TANZANIAN PROJECTS IN THE NEXT 10 YEARS

UWT YATOA MSAADA WA VIFAA TIBA HOSPITALI YA RUFAA DODOMA