Benki ya NMB imetoa udhamini wa Sh milioni 100 kwa ajili ya kusaidia maandalizi na uendeshaji wa Mkutano Mkuu wa 40 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) utakaofanyika jijini Arusha. Udhamini huo unaongeza nguvu katika maandalizi ya mkutano huo muhimu unaotarajiwa kuwakutanisha wajumbe kutoka mamlaka mbalimbali za serikali za mitaa nchini.
Makabidhiano ya mfano wa hundi hiyo yalifanywa na Meneja wa NMB Kanda ya Kaskazini, Baraka Ladislaus, kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya mkutano huo, Juma Hokororo, katika hafla iliyoshuhudiwa na Kaimu Katibu Mkuu wa ALAT, Thomas Vungwa. Msaada huo unalenga kuchangia kufanikisha mkutano huo wa uchaguzi pamoja na maandalizi yake kwa ujumla.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Baraka alisema NMB imeendelea kuwa mshirika wa ALAT kwa zaidi ya miaka 10, jambo linalotokana na kutambua mchango wa jumuiya hiyo katika kusukuma maendeleo kupitia serikali za mitaa.
Alisema benki hiyo itaendelea kuunga mkono juhudi zinazosaidia kuimarisha taasisi zinazogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.
Kwa upande wake, Hokororo aliishukuru NMB kwa mchango huo, akisema umefika kwa wakati muhimu kuelekea mkutano huo wa kitaifa. Alisema ushiriki wa wadau kama NMB unaendelea kuwa nguzo muhimu katika kufanikisha mkutano wa ALAT, ambao ni jukwaa muhimu kwa uchaguzi wa viongozi na mjadala wa masuala ya maendeleo ya serikali za mitaa.
Meneja wa benki ya NMB Kanda ya kaskazini Baraka Ladislaus (wa pili kulia) akimkabidhi mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya mkutano wa jumuiya ya tawala za mitaa taifa (ALAT) Juma Hokororo mfano wa hundi ya sh100 milioni waliyotoa kudhamini mkutano wa uchaguzi wa jumuiya hiyo, ikishuhudiwa na kaimu katibu mkuu wa ALAT Thomas Vungwa (wa pili kushoto) na Amanda Feruzi Meneja Mwandamizi Biashara za Serikali Benki ya NMB.



Comments