COSOTA YATAJA MAFANIKIO LUKUKI AWAMU YA RAIS SAMIA


 Afisa Mtendaji Mkuu na Msimamizi wa Hakimiliki (COSOTA), Doreen Sinare akizungumza na waandishi wa habari, kwenye Ukumbi wa Idara ya Habari MAELEZO, Dodoma, kuhusu mafanikio na mwelekeo wa ofisi hiyo ndani ya miaka minne ya uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita.


TAARIFA YA MAFANIKIO YA MIAKA MINNE YA SERIKALI YA AWAMU YA SITA YA MHESHIMIWA DKT. SAMIA SULUHU HASSAN RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

  

OFISI YA HAKIMILIKI TANZANIA (COSOTA)

 

Katika kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ofisi ya Hakimiliki Tanzania (COSOTA) imefanikiwa kwa kiasi kikubwa na yamefanyika mambo mengi yaliyosaidia kuimarisha usimamizi wa hakimiliki nchini.

 

Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipolihutubia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mara ya kwanza baada ya kuingia madarakani aliahidi kuimarisha usimamizi wa hakimiliki na kuhakikisha Wasanii wananufaika zaidi na kazi zao pamoja na kupata mirabaha na ametekeleza.

 

Kati ya mambo yaliyofanyika ni pamoja na marekebisho katika Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki Na. 7 ya mwaka 1999 yaliyofanyika mwaka 2022 na 2023 kupitia Sheria za Fedha za mwaka 2022 na 2023.

 

Mabadiliko haya makubwa yalianzisha chanzo kipya cha mapato cha tozo ya hakimiliki (copyright levy), ambapo vifaa vinavyotumika kusambaza, kuzalisha na kuhifadhi kazi za sanaa na fasihi hutozwa asilimia moja nukta tano (1.5%) kila vinapoingia, kuzalishwa au kuundwa hapa nchini. Fedha hizo hukusanywa kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Lengo kuu la kuanzishwa kwa tozo hiyo ni kuwajengea uwezo wa kiuchumi wadau wa sanaa na uandishi nchini wakiwemo wasanii, waandishi na wabunifu ambao kwa muda mrefu kazi zao zimekuwa zikitumika katika mazingira mbali mbali ya kijamii kama vile kuhifadhi, kubebea na kusambaza kazi sanaa na uandishi na kuwanufaisha wadau wengine pamoja na watu binafsi bila ya wenye kazi kupata haki zao.

Marekebisho hayo ya Sheria yaliweza kuweka asilimia 1.5 kwa baadhi ya orodha ya vifaa yaani Radio/TV set enabling recording, analogue audio recorders, analogue video recorders, CD/DVD copier, digital jukebox, MP 3 player, CD, DVD, Vinyl, Mini Disc na SD Memory ili kuweza kulipishwa tozo hiyo ambapo ni vifaa 13 kati ya vifaa 25 vilivyoombwa.

 

Kupitia Kanuni ya Tozo ya Hakimiliki “The Copyright and Neighbouring Rights (copyright Levy on blank devices) Regulations, 2023 GN No.378 published on 2/6/2023 (English) na GN No.385 published on 2/6/2023” mapato hayo yalianza kukusanywa.

 

Kupitia chanzo hiki, COSOTA imekusanya jumla ya Tshs. 1,428,105,241.44 kuanzia Septemba, 2023 hadi Februari, 2025 ambapo Ofisi imefanikiwa kupokea fedha za tozo ya hakimiliki za mwaka wa fedha 2023/2024 kutoka Wizara ya Fedha kiasi cha Tshs. 847,985,594.26.

 

Aidha, Ofisi imeona kuwa vifaa vilivyowekwa kwenye Sheria havitoshi kwani vingi vimepitwa na wakati na havitumiki sana kama ilivyo kwa baadhi ya vifaa vilivyoachwa, hivyo kuna haja ya kuongeza baadhi ya vifaa hasa simu, Computers, External drives, printers, scanner, tablets, photocopier, printing plates na flash disks ili kuhakikisha kuwa malengo ya kuwepo kifungu hiki yanafikiwa lakini pia itaongeza mapato kwa Serikali na kwa wabunifu nchini.

 

Kwa mujibu wa Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki pamoja na Mabadiliko Sheria ya Fedha Na. 5 ya mwaka 2022, kiasi cha tozo ya Hakimiliki kilichokusanywa ndani ya mwaka husika hugawanywa kwa makundi manne katika asilimia kama ifuatavyo: COSOTA 20%, Mfuko wa Utamaduni 10%, Mfuko Mkuu wa Serikali 10%, na Kampuni za kukusanya na kugawa mirabaha (CMOs) kwa ajili ya wasanii, waandishi na wamiliki wengine wa hakimiliki 60%.

 

Mgawanyo wa Makusanyo ya Tozo ya Hakimiliki kwa Mwaka        2023/24 na 2024/25

Na

Mwaka

Jumla ya Makusanyo

COSOTA (Asilimia 20)

Mfuko Mkuu wa Serikali (Asilimia 10)

Mfuko wa Utamaduni (Asilimia 10)

CMOs (Asilimia 60)

1.

2023/2024

 847,985,594.26

 169,597,118.85

 84,798,559.43

 84,798,559.43

 508,791,356.56

2.

2024/2025

(Julai – Februari, 2025)

 580,119,647.18

 116,023,929.44

 58,011,964.72

 58,011,964.72

 348,071,788.31

 

JUMLA

 1,428,105,241.44

 285,621,048.29

 142,810,524.14

 142,810,524.14

 856,863,144.86

 

Aidha, Ofisi imeandaa mgao wa mapato haya kama mirabaha kutokana na fedha za tozo ya hakimiliki utakaofanyika hivi karibuni. Mgao huu unategemewa kunufaisha makundi ya kazi za muziki, filamu, maandishi, sanaa za ufundi na sanaa za maonesho – Kila daraja litapata kiwango sawa na madaraja mengine.

Kiasi cha Tsh. 508,791,356.56 kitagawiwa kwa wasanii ambacho ni asilimia sitini (60%) ya tozo ya hakimiliki, na kiasi cha Tsh. 84,798,559.43 (asilimia 10) kinaenda Mfuko wa Sanaa na Utamaduni ambapo fedha hizo pia ni kwa ajili ya wasanii. Hivyo wasanii na waandishi watanufaika na jumla ya kiasi cha Tsh. 593,589,915.98 zilizokusanywa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024. Gawio la Serikali ni 142,810,524.14 na gharama ya uendeshaji COSOTA ni 285,621,048.29.

Pia mabadiliko hayo ya Sheria yamepelekea muundo wa COSOTA kubadilika na kuruhusu uanzishwaji wa Makampuni ya Wasanii ya kukusanya na kugawa mirabaha (Collective Management Organization - CMO) na COSOTA kubaki kama msimamizi wa masuala ya hakimiliki na kusimamia Kampuni hizo.

Marekebisho ya Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki ya mwaka 2022 yalipelekea kuandaliwa kwa Kanuni ya Kuanzishwa kwa Makampuni ya kukusanya na kugawa Mirabaha  na kuruhusu uanzishwaji wa Makampuni  kwa ajili ya kusimamia haki mbalimbali za aina za kazi za Sanaa na Uandishi - Kanuni za Hakimiliki na Hakishiriki (Kampuni za Ukusanyaji na Ugawaji Mirabaha), kupitia tangazo la Serikali Na. 215 la tarehe 24 Machi, 2023 na Copyright and Neighbouring Rights (Royalty Collection and Distribution Collective Management Organisations), Government Notice No. 211 published on 24/3/2023).

 

Katika kuimarisha dhana ya kuhakikisha wasanii na waandishi wananufaika zaidi na kazi zao, baada ya mabadiliko ya Sheria ya mwaka 2022, COSOTA ilitoa leseni ya kukusanya na kugawa mirabaha ya daraja la muziki kwa Kampuni ya Tanzania Music Rights Society (TAMRISO) mnamo mwezi Julai 2023. Na Kampuni hiyo ilianza ukusanyaji wa fedha za mirabaha mnamo mwezi Januari 2024 mpaka 16 Novemba, 2024 kwa mujibu wa vigezo vya leseni hiyo.

Kwa kipindi hicho TAMRISO ilikusanya kiasi cha Tshs. 256,448,440.00 kupitia baa, hoteli, kumbi za starehe, kumbi za sherehe, migahawa, maduka ya biashara nk. Katika makusanyo hayo asilimia sabini (70%) baada ya malipo ya kodi ya serikali (18% VAT) sawa na Tshs. 147,201,405 ndiyo zitagawiwa kwa wasanii wa muziki na asilimia thelathini (30%) baada ya malipo ya kodi ya serikali (18% VAT) ni kwa ajili ya uendeshaji wa shughuli za kiutawala TAMRISO.

Aidha, hatua mbalimbali zinafanyika kupitia COSOTA, wasanii, waandishi na wadau wengine ili kuanzishwa kwa Kampuni nyingine kwa aina nyingine za kazi kama vile filamu, muziki, Sanaa za ufundi, Sanaa za maonesho na uandishi.  

Katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, usajili wa kazi zinazolindwa na Sheria ya hakimiliki na hakishiriki umeongezeka kwa asilimia 70 Ukilinganisha na miaka ya nyuma ambapo kuanzia mwaka 2021 mpaka Februari 2025, COSOTA, imesajili kazi za Sanaa na uandishi 11,519 na Wabunifu 3,436. Idadi hii ya wabunifu pamoja na kazi zao imetokana na zoezi la utoaji wa elimu na mafunzo mbalimbali ya hakimiliki na usajili kupitia vyombo vya habari, mitandao ya kijamii, semina lakini pia kushiriki matukio mbalimbali ya wadau ambapo COSOTA ilipata fursa ya kuelimisha wadau kuhusiana na hakimiliki na uhamasishaji wa usajili wa kazi za hakimiliki.

 

Halikadhalika, katika kipindi hicho kamati maalumu ya Usajili ndani ya COSOTA inayojihusisha na masuala ya usajili, imefanikiwa kutoa mafunzo na ufafanuzi kuhusiana na hakimiliki kwenye kazi zilizopokelewa katika kipindi hicho kwa idadi ya wabunifu 167.

 

Vilevile, katika kipindi cha miaka minne ya serikali ya awamu sita COSOTA imetoa jumla ya vyeti 7,679 vya uthibitisho wa umiliki wa hakimiliki kwa wabunifu waliosajili kazi zao.

Kwa mwaka 2021 - 2025 COSOTA imefanikiwa kufanya migao miwili kama alivyoahidi Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan alipolihutubia bunge mwaka 2021 ambapo alisisitiza katika kipindi cha uongozi wake, serikali itahakikisha wabunifu wote wananufaika zaidi na kazi zao. Mgao wa kwanza ambao ulikuwa ni mgao wa ishirini na tatu ulifanyika tarehe 28/01/2022 na ulikuwa wa kiasi cha Tshs. Tshs. 312,290,259,000, ambapo Wasani 1,123 walinufaika, na ulitokana na matumizi ya kazi 5,924 za muziki ambazo zilitumika katika vituo 11 vya redio, ikiwemo redio katika ngazi ya kitaifa, Mkoa, wilaya, kijamii na za kidini.

Mgao wa pili katika kipindi cha serikali ya awamu ya sita ulifanyika tarehe 21/07/2023 na ulikuwa ni mgao wa ishirini na nne wa mirabaha kwa kazi za muziki na COSOTA iligawa kiasi cha Tshs. 396,947,743.20 na wasanii wa muziki 8,165 walinufaika kupitia kazi zao 61,490.

Hivi ni viwango vikubwa zaidi kuwahi kufanyika katika migao ya mirabaha ambayo COSOTA imekuwa ikigawa kwa miaka ya nyuma kabla ya uongozi huu wa serikali ya awamu ya sita ambao ulianzisha kampeni ya kusisitiza watumiaji wa kazi za Sanaa katika maeneo ya biashara kulipia matumizi ya kazi hizo.

Pamoja na hayo uongozi wa Dkt. Samia umefanya mageuzi makubwa ya kibajeti kwa COSOTA kwa lengo la kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya Ofisi kwa kutoa fedha za serikali kiasi cha Tshs. 1.5 bilioni. Fedha hizo zimesaidia kuboresha usimamizi wa hakimiliki nchini, ununuzi wa vitendea kazi na utoaji elimu ya hakimiliki pamojana ujenzi wa mfumo wa usajili.

Halikadhalika, katika kuhakikisha tasnia ya hakimiliki nchini inaimarika serikali ya awamu ya Sita kupitia uongozi wa Dkt. Samia COSOTA imepata ufadhili wa mradi wa Mpango wa Kuwezesha Mazingira ya Biashara (MKUMBI) unaosimamiwa na Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya wenye lengo la kuboresha mazingira ya biashara. Mradi hii umewezesha COSOTA kupata ufadhili kwa ajili ya kutoa elimu ya uharamia na hakimiliki kwa kazi za ubunifu, kuboresha mfumo wa COSOTA na kunganisha mifumo ya COSOTA, Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA)  na Bodi ya Filamu Tanzania (TFB) ili iweze kusomana pamoja na kuandaa Kanuni za utekelezaji wa Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki, zinazohusu usajili wa kazi zinazolindwa na Sheria ya Hakimiliki, zinazohusu Watu wenye uoni hafifu na wasioona kuweza kupata machapisho na zinazohusu haki ya Kunufaika na Mauzo Endelevu (resale rights).

Fauka ya hayo, katika kipindi cha miaka minne ya uongozi Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Julai 2022 iliundwa Kamati maalum ya Kuratibu Ukusanyaji wa maoni ya namna bora ya kusimamia hakimiliki nchini iliyokuwa na wadau mbalimbali wakiwepo wasanii na waandishi iliyoongozwa na Mwenyekiti Bw. Victor Tesha pamoja na Mheshimiwa Hamis Mwinjuma (Mb) Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo (kabla hajateuliwa katika nafasi ya Waziri) ilifanya kazi ya kukusanya maoni ya wadau wa hakimiliki katika Kanda tano nchini. Taarifa ya Kamati hiyo ilionesha umuhimu wa kuendelea kutoa elimu, kusimamia masuala ya uharamia, kubadili muundo wa COSOTA na kuongeza idadi ya watumishi pamoja na kusimamia kukamilika kwa mchakato wa kuanzishwa kwa Kampuni za kukusanya na kugawa mirabaha ambazo husimamiwa na wasanii wabunifu wenyewe na COSOTA kubaki msimamizi wa Kampuni hizo. Taarifa hiyo imefanyiwa kazi utekelezaji wake na kupelekea nabadiliko mbalimbali katika tasnia ya hakimiliki.

Kwa kipindi cha miaka minne ya serikali ya awamu ya sita COSOTA imefanikiwa kupokea  jumla ya migogoro 136 na kusuluhisha migogoro 118. Migogoro 10 kati ya hiyo haikumalizika na ilifunguliwa kesi mahakamani na migogoro 8 inaendelea COSOTA. Sambamba na migogoro hii, COSOTA imehusika na kesi za hakimiliki 10.

 

Pia katika kipindi hicho maandiko ya Itifaki za Kimataifa yaani Itifaki ya Kampala yaani Kampala Protocol on Voluntary Registration of Copyright and Related Rights 2021, Itifaki  ya Beijing yaani Beijing Treaty on Audivisial Perfomances na Maandiko ya Mikataba ya Internet yaani Internet Reaties ya WIPO Copyright Treaty (WCT) ya mwaka 1996 na WIPO Performances and Phonograms Treaty (WPPT) ya mwaka 1996 iliandaliwa na kikao cha kuwakutanisha wadau wa Sanaa katika madaraja mbalimbali na kuwaelimisha wadau kuhusu Itifaki hiyo na faida ambazo zinapatikana baada ya Tanzania kuiridhia imefanyika na sasa ushirikishaji unaendelea ili kuhakikisha kuwa Tanzania inaridhia mikataba hii mapema iwezekanavyo ili kuboresha mazingira ya ulinzi na biashara ya kazi za hakimiliki.

 

Katika kipindi hiki cha Serikali ya awamu ya Sita Ofisi ilifanikiwa kuendesha Semina ya kujengeana uwezo kuhusu masuala ya hakimiliki na Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki kwa makundi mbalimbali wakiwepo mahakama, bunge, wahariri, vyuo vikuu, mashirikisho na vyama vywa waandishi na wasanii na mawakili wasio wa serikali.

Hata hivyo katika kipindi cha serikali ya awamu ya sita kupitia uwezeshwaji wa kibajeti Ofisi imefanikiwa kutoa elimu ya hakimiliki kuhusu mikataba, usajili wa kazi, uhamasishaji wa ulipaji wa mirabaha, kupambana na uharamia kwa kuandaa semina, kushiriki maonyesho mbalimbali, vipindi vya redio na televisheni na midahalo. Elimu hiyo imetolewa kwa Mikoa ya Mbeya, Mwanza, Morogoro, Dodoma, Mtwara, Arusha, Dar es Salaam, Pwani, Tanga, na Ruvuma. pia Ofisi ilifanikiwa kutoa matangazo ya kukemea uharamia, kuhamasisha ulipaji wa mirabaha na kutumia mitandao ya kijamii kutoa elimu na kusambaza taarifa mbalimbali kwa umma.

Halikadhalika, katika kipindi hicho kumekuwa na kuimarika kwa mahusiano na mashirika ya kimataifa yaliyochangia kupelekea utaratibu mahususi kuanza wa kuanzishwa kwa Kituo cha kutoa Elimu ya Hakimiliki cha Intellectual Property Training Institution (IPTI). Kituo hicho kitaanzishwa kwa ufadhili wa Shirika la Miliki Bunifu Duniani (WIPO) kwa usimamizi wa taasisi zinazosimamia masuala ya hakimiliki (copyright) na Miliki Bunifu za Viwanda (Industrial Property) kwa Tanzania. Hii imetekelezwa kwa pamoja na kusainiwa kwa makubaliano ya pamoja baina ya Ofisi ya Hakimiliki Tanzania (COSOTA), Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Ofisi ya Hakimiliki Zanzibar (COSOZA) na Wakala wa Usajili Biashara na Mali Zanzibar (BPRA). Kituo hicho kitakuwa kikitoa mafunzo ya miliki ubunifu ya muda mfupi kutokana na mahitaji ya makundi mbalimbali.

Sambamba na hili, kupitia mashirikiano na uridhiwaji wa Itifaki ya Marakesh yaani Marrakesh Treaty to Facilitate Access to Published Works for Persons Who Are Blind, Visually Impaired or Otherwise Print Disabled, Tanzania kupitia Taasisi ya Chama cha Wasiiona Tanzania (Tanzania League of the Blind -TLB) imenufaika kwa kupata vifaa vya VEVO 10 Daisy na mafunzo ya matumizi ya vifaa hivyo kutoka Shirika la Miliki Ubunifu Duniani la WIPO kwa Shule sita na Chuo kimoja cha wenye uoni hafifu na wasioona kama ifuatavyo Tanga - Shule ya Sekondari ya Wasichana Korogwe, Dar es Salaam - Shule ya Uhuru Mchanganyiko,  Shule ya Sekondari Lugalo, Shule ya Msingi Toangoma, Ruvuma - Shule ya Msingi Ruhila, Tabora - Shule ya Msingi Furaha, na Chuo cha Ufundi Mtwara kwa ajili ya kuwawezesha kurekodi wakati walimu wanafundisha na kuweka masomo katika mfumo unaowawezesha kusoma.  

 

Pamoja na mafanikio hayo, mnamo Januari 2025 COSOTA ilisaini makubaliano na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) ili kulipia leseni kutokana na matumizi ya kazi za muziki kwenye viwanja vya ndege ili wasanii wa muziki wanufaike na matumizi ya kazi zao.

                                                                                             

Pia kwa kuzingatia ulinzi wa kazi za ubunifu katika kipindi cha serikali ya awamu ya sita COSOTA ilifanya Operesheni  mbalimbali za kupambana na Uharamia katika mitandao na katika mikoa ya Dar es Salaam, Kagera, Dodoma, Tabora, Shinyanga, Songwe, Mwanza, Morogoro, Arusha, Kilimanjaro, Lindi, Mtwara, Manyara na Mara Ikiwa ni utekelezaji wa Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki ya mwaka 1999, kanuni ya uzalishaji na usambazaji ya Mwaka 2006 na kanuni ya Ufifilishaji wa makosa ya Hakimiliki ya mwaka 2020.

 

Katika kipindi cha serikali ya awamu ya sita Muziki wa singeli ambao ni wa kipekee kutoka Tanzania umekuwa kwa kasi na kupendwa naidi nchini na kuvuka mipaka ya nchi. Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano alieleza namna alishuhudia wazungu wakifurahia Muziki huo. Katika kipindi hiki, COSOTA imetoa elimu kwa Wasanii, watayarishaji, wafanyabiasha na wadau wa Singeli kwa kushirikiana na Taasisi isiyo ya kiserikali ya Uswazi Got Talent na Kandoro Baba Entertainment chini ya Meneja Kandoro na Kituo cha cha redio na televisheni kupitia Efm kikiendeshwa na Samio Love kuwaeleza umuhimu wa usajili wa kazi zao na faida za kusajili ambapo takribani wasanii 20 wa Muziki wa Singeli wamesajili kazi zao COSOTA. Pia wamenufaika na mgao wa mirabaha kwa mwaka 2022 na mwaka 2023 na nimategemeo yetu kuwa watanufaika Zaidi kutokana na kupendwa na kushiriki katika biashara ya muziki wa singeli ndani nan je ya nchi.

 

Ni matarajio ya COSOTA kuwa mafanikio haya ni chachu ya ukuaji wa biashara ya tasnia ya hakimiliki sasa na miaka ijayo ambapo yataongeza kipato kwa wasanii, waandishi na wabunifu wenye hakimiliki na kutengeneza ajira zaidi sambamba na kuongeza pato la taifa. Kazi iendelee!

 

                    

 

                        ****ASANTENI KWA KUNISIKILIZA*****

 

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MWABUKUSI ATOA NENO SIMBA KUSUSIA DERBY DHIDI YA YANGA

RAIS TRUMP ARARUANA NA RAIS WA UKRAINE

SERIKALI YALIKUBALI OMBI LA DIAMOND

MWANAMKE ALIYEVUNJA REKODI KWA KUZAA WATOTO 69

HOSPITALI YA MUHIMBILI YAANZISHA HUDUMA YA KISASA YA KUZIBA MAPENGO

ARAJIGA AULA KOMBE LA DUNIA

BODI YA LIGI YAKIRI MAKOSA, WAIOMBA YANGA WAYAMALIZE