Historia mpya ya uchumi inaandikwa Kusini mwa Tanzania baada ya Serikali kuthibitisha kuwa ujenzi wa Bandari ya Mbambabay yenye thamani ya shilingi bilioni 80 umefikia asilimia 47, hatua inayoiweka Nyasa kwenye mstari wa kuwa kitovu kipya cha biashara ya kikanda.
Akikagua mradi huo, hivi karibuni Waziri wa Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa alisema bandari hiyo ni ya kimkakati kwa Taifa na imebuniwa kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi kwa zaidi ya miaka 50. Tayari nguzo 81 kati ya 140 zimewekwa, huku kukamilika kwake kukitarajiwa Agosti 2026.
Mradi huo unatarajiwa kufungua fursa za ajira, kupunguza gharama za usafirishaji na kuunganisha masoko ya Malawi, Msumbiji na ukanda wa SADC. Bandari itakuwa na uwezo wa kuhudumia meli mbili za tani 5,000 pamoja na miundombinu ya kisasa ya kuhifadhi na kushughulikia mizigo.
Wakazi wanasema mradi huo utabadilisha maisha yao. “Itatuwezesha kuuza samaki na mazao nje ya nchi,” anasema mvuvi Martin Challe, huku mkulima Agatha Samata akitabiri ongezeko la wawekezaji na bei bora za mazao.
Mbambabay inaonekana kuwa mlango mpya wa biashara na alama ya mabadiliko makubwa ya Ruvuma.




Comments