DKT. MAFUMIKO AELEZA TARATIBU ZA KUPIMA VINASABA (DNA)

 Mkemia Mkuu wa Serikali, Dkt. Fidelice  Mafumiko, amesema kuwa Ofisi hiyo inaendelea kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia misingi ya sheria mbalimbali zinazosimamia mamlaka hiyo.

Dkt. Mafumiko ameyasema hayo Februari 11, 2026, alipokuwa akizungumzia mafanikio ya mamlaka hiyo tangu kuanza kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan katika mkutano na vyombo vya habari uliofanyika kwenye Ukumbi wa Idara ya Habari MAELEZO jijini Dodoma Machi 11, 2026.

Alieleza kuwa utekelezaji wa majukumu yao unaongozwa na sheria tatu kuu, ikiwemo Sheria ya Usimamizi wa Vinasaba vya Binadamu. Alifafanua kuwa sheria hiyo imeweka utaratibu maalum unaofuatwa katika huduma ya upimaji wa vinasaba, ambapo mamlaka hiyo imeandaa kanuni zinazoongoza mchakato huo.

Kupitia kanuni hizo, kumeanzishwa utaratibu unaoitwa mamlaka ombezi, unaoweka wazi namna maombi ya vipimo vya vinasaba yanavyopaswa kuwasilishwa ili kuhakikisha uwajibikaji na uhalali wa maombi hayo.

Dkt. Mafumiko alisema kuwa mtu anayehitaji kupima vinasaba hatakiwi kufika moja kwa moja katika ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali kuwasilisha ombi lake.

Alieleza kuwa kama ombi linahusiana na masuala ya jinai, mamlaka ya kuwasilisha maombi hayo yapo kwa Jeshi la Polisi au Mahakama.

Hata hivyo, iwapo ni ombi la kijamii kama vile kuthibitisha uhalali wa mzazi kwa mtoto, jukumu hilo hutekelezwa na maafisa ustawi wa jamii wanaotambulika au wakili aliyesajiliwa ambaye anaweza kuandika barua rasmi kwa niaba ya mteja wake.


Aidha, alisema baada ya kukamilika kwa taratibu zote za maombi, mwombaji hupatiwa taarifa ya gharama za huduma hiyo. Kwa sasa, ada iliyopitishwa na Bodi ya Wakurugenzi nishilingi laki mbili na na kumi na mbili ( 212,000) kwa mtu anayetoa sampuli moja ya kipimo cha vinasaba.


Alisisitiza kuwa utaratibu huo umewekwa ili kuhakikisha huduma inatolewa kwa kuzingatia sheria, uwazi na ulinzi wa haki za wahusika wote.








 

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

Kizza Besigye ‘akamatwa’ tena Uganda

Wasifu wa Kizza Besigye

IRAN YAMTANGAZA AYATOLLAH MPYA

KILA MWANAMKE ANAPASWA KUFAHAMU HII...

MBUNGE DKT. MAJULE ATOA MSAADA WA VYAKULA, VYANDARUA 100 SHULE YA VIZIWI DODOMA

KWA KHERI MAKARANGA UMEUTIMIZA MWENDO...

MAMBO MADOGO YANAYOVUTIA KWA MPENZI WAKO

KWA NINI MAASKOFU JANA KWENYE IBADA YA KUMUAGA PENGO WALIVAA MAVAZI MEUPE WAKATI NI MSIBA..?

DKT. MAJULE AKABIDHIWA CHETI CHA SHUKRANI UWT DODOMA KUFANIKISHA USHINDI WA CCM 2025