BAADA ya kufanya uzinduzi wa kampeni kwenye Uwanja wa Tanganyika Packers, Kawe ijini Dar es Salaam Agosti 28, 2025, leo Septemba 28, 2025 Mgombea wa Kiti cha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Samia Suluhu Hassan anaingia kwa kishindo mkoa wa Pwani ukiwa ni Mkoa wa 16 baada ya kufanikisha kwa kiwango kikubwa kampeni katika mikoa mingine 15.
Tanzania Bara ni; Morogoro, Dodoma, Songwe, Mbeya, Njombe, Iringa, Singida, Tabora, Kigoma, Ruvuma, Lindi na Mtwara.
Tanzania Visiwani; Mkoa wa Kusini Unguja, Mkoa wa Kaskazini Unguja, Mkoa wa Kusini Pemba.
Bado mikoa ya; Dar es Salaam,Tanga, Kilimanjaro, Arusha, Manyara, Rukwa, Katavi, Shinyanga, Simiyu, Geita, Mara, Kagera, Mwanza, Mkoa wa Mjini Magharibi na Mkoa wa Kaskazini Pemba
Akiwa katika mikutano hiyo, Dkt. Samia anajinadi kwa kuelezea mafanikio makubwa ya maendeleo yaliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita katika mikoa hiyo, pia hutoa ahadi ya utekelezaji wa miradi mbalimbali.
Aidha, Dkt. Samia amekuwa akisisitiza kudumisha Muungano na kuendelea kulinda amani na utulivu hasa katika kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu, ambapo pia amewatoa wananchi wasiwasi kwamba hakutokuwa na vurugu kwani vyombo vyote vya ulinzi na usalama viko imara, hivyo siku ya Uchaguzi Mkuu Oktoba 29 mwaka huu wajitokeze kwa wingi tena bila hofu kwenda kupiga kura na kurejea salama majumbani.
Pamoja na kuelezea kwa undani Ilani ya uchaguzi ya chama hicho, Dkt. Samia ambaye mgombea wake mwenza ni Dkt. Emmauel Nchimbi, atatumia fursa hiyo kujinadi yeye, wagombea ubunge na madiwani wa chama hicho.
Akiwa katika Mkoa huo Pwani, atafanya mikutano ya kampeni katika miji ya Kibaha, Chalinze na Msata, hatimaye kupiga hodi Mkoa wa 16 wa Tanga.
Comments