Eid El-Fitri ni miongoni mwa sikukuu kubwa na zenye heshima kubwa katika Uislamu, ikija mara moja kila mwaka baada ya kukamilika kwa mwezi mtukufu wa Ramadhani. Ni siku ya furaha, shukrani na mshikamano kwa Waislamu duniani kote baada ya mwezi mzima wa ibada, kujinyima na kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu.
Katika siku hii muhimu, Waislamu husherehekea kwa nyoyo zilizojaa furaha, wakikumbuka mafanikio ya kufunga na kufanya ibada mbalimbali. Pia ni wakati wa kuimarisha mahusiano ya kifamilia na kijamii kupitia ziara, sadaka na kushirikiana chakula.
Kwa wengi, Eid ni zaidi ya sherehe; ni siku ya kuonesha ucha Mungu, upendo na mshikamano kwa jamii. Watu huvaa nguo nzuri, kuandaa vyakula maalum na kuwakaribisha ndugu, jamaa na marafiki.
Hata hivyo, pamoja na furaha yake, siku ya Eid pia ina taratibu na mambo muhimu ambayo Muislam anapaswa kuyazingatia ili kuhakikisha anaitimiza kwa mujibu wa mafundisho ya dini ya Kiislamu.
Katika mataifa haya ya Ghuba, imeelezwa kuwa Eid El-Fitri itasherehekewa siku ya Ijumaa, Machi 20, 2026, baada ya kamati za kuandama mwezi kuthibitisha kuwa mwezi haukuonekana mapema, hivyo Ramadhani kukamilika kwa siku 30.
Kwa ujumla, Waislamu duniani kote wanatarajia kusherehekea siku ya Eid kuanzia kesho na baadhi ya nchi keshokutwa, ingawa mara nyingi hutokea utofauti wa tarehe kutokana na tofauti za uandamaji wa mwezi na maamuzi ya mamlaka za Kiislamu katika nchi husika.
Kwa upande wa Afrika Mashariki, Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) lilitangaza kuwa Eid inaweza kuwa Ijumaa au Jumamosi kutegemea kuandama kwa mwezi. Kuanzia Alhamisi, Machi 19, Waislamu wanaanza kuufuatilia mwezi; ukiandama basi Ijumaa itakuwa Eid, na usipoonekana basi itakuwa Jumamosi. Hali hii pia inafanana na nchi kama Kenya, Uganda, Somalia na Sudan ambapo baadhi ya Waislamu wamefunga siku 29 na wengine 30.



Comments