MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa tahadhari ya mvua kubwa kwa baadhi ya maeneo ya mikoa 20 nchini. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na TMA, leo Jumamosi 27 Desemba 2025 imetaja mikoa hiyo kuwa ni Arusha, Kilimanjaro, Manyara, Kigoma, Katavi, Singida, Dodoma, Rukwa, Songwe, Mbeya, Iringa, Njombe, Morogoro, Ruvuma, Tanga, Dar es Salaam, Lindi, Mtwara na Pwani ikijumuisha visiwa vya Mafia. TMA imesema mvua hizo zinatarajiwa kunyesha Jumapili, 28 Desemba 2025, na huenda zikasababisha madhara mbalimbali ikiwamo mafuriko, maporomoko ya udongo na usumbufu wa shughuli za kiuchumi na kijamii. Wananchi wanaoishi katika maeneo yaliyotajwa, hususan walioko mabondeni na maeneo hatarishi, wametakiwa kuchukua tahadhari za mapema ili kuepuka athari zinazoweza kujitokeza kutokana na mvua hizo. TMA imewasisitiza wananchi kuendelea kufuatilia taarifa na utabiri wa hali ya hewa unaotolewa mara kwa mara ili kupata taarifa sahihi na za wakati.
- Get link
- X
- Other Apps